[1] Msifuni BWANA. Lisifuni jina la BWANA, msifuni, enyi watumishi wa BWANA, [2] ninyi ambao mnatumika ndani ya nyumba ya BWANA, katika nyua za nyumba ya Mungu wetu. [3] Msifuni BWANA, kwa kuwa BWANA ni mwema, liimbieni sifa jina lake, kwa maana hilo lapendeza. [4] Kwa maana BWANA amemchagua Yakobo kuwa wake mwenyewe, Israeli kuwa mali yake ya thamani. [5] Ninajua ya kuwa BWANA ni mkuu, kwamba Bwana wetu ni mkuu kuliko miungu yote. [6] BWANA hufanya lolote apendalo, mbinguni na duniani, katika bahari na vilindi vyake vyote. [7] Hufanya mawingu kupanda kutoka miisho ya dunia; hupeleka umeme wa radi pamoja na mvua na huleta upepo kutoka ghala zake. [8] Alimuua mzaliwa wa kwanza wa Misri, mzaliwa wa kwanza wa wanadamu na wanyama. [9] Alipeleka ishara zake na maajabu katikati yako, ee Misri, dhidi ya Farao na watumishi wake wote. [10] Aliyapiga mataifa mengi, na akaua wafalme wenye nguvu: [11] Mfalme Sihoni na Waamori, Ogu mfalme wa Bashani na wafalme wote wa Kanaani: [12] akatoa nchi yao kuwa urithi, urithi kwa watu wake Israeli. [13] Ee BWANA, jina lako ladumu milele, kumbukumbu za fahari zako, Ee BWANA, kwa vizazi vyote. [14] Maana BWANA atawathibitisha watu wake, na kuwahurumia watumishi wake. [15] Sanamu za mataifa ni fedha na dhahabu, zilizotengenezwa kwa mikono ya wanadamu. [16] Zina vinywa, lakini haziwezi kusema, zina macho, lakini haziwezi kuona; [17] zina masikio, lakini haziwezi kusikia, wala hakuna pumzi katika vinywa vyao. [18] Wale wanaozitengeneza watafanana nazo, vivyo hivyo wale wote wanaozitumainia. [19] Ee nyumba ya Israeli, msifuni BWANA; ee nyumba ya Aroni, msifuni BWANA; [20] ee nyumba ya Lawi, msifuni BWANA; ninyi mnaomcha, msifuni BWANA. [21] Msifuni BWANA kutoka Sayuni, msifuni yeye aishiye Yerusalemu. Msifuni BWANA.