[1] Ninampenda BWANA kwa maana amesikia sauti yangu; amesikia kilio changu ili anihurumie. [2] Kwa sababu amenitegea sikio lake, nitamwita siku zote za maisha yangu. [3] Kamba za mauti zilinizunguka, maumivu makuu ya kuzimu yalinipata, nikalemewa na taabu na huzuni. [4] Ndipo nikaliitia jina la BWANA: “Ee BWANA, niokoe!” [5] BWANA ni mwenye neema na haki, Mungu wetu ni mwingi wa huruma. [6] BWANA huwalinda wanyenyekevu, nilipokuwa katika shida kubwa, aliniokoa. [7] Ee nafsi yangu, tulia tena, kwa kuwa BWANA amekuwa mwema kwako. [8] Kwa kuwa wewe, Ee BWANA, umeniokoa nafsi yangu na mauti, macho yangu kutokana na machozi, miguu yangu kutokana na kujikwaa, [9] ili niweze kutembea mbele za BWANA, katika nchi ya walio hai. [10] Niliamini, kwa hiyo nilisema, “Mimi nimeteseka sana.” [11] Katika taabu yangu nilisema, “Wanadamu wote ni waongo.” [12] Nimrudishie BWANA nini kwa wema wake wote alionitendea? [13] Nitakiinua kikombe cha wokovu na kulitangaza jina la BWANA. [14] Nitazitimiza nadhiri zangu kwa BWANA mbele za watu wake wote. [15] Kifo cha watakatifu kina thamani machoni pa BWANA. [16] Ee BWANA, hakika mimi ni mtumishi wako, mimi ni mtumishi wako, mwana wa mjakazi wako; umeniweka huru toka katika minyororo yangu. [17] Nitakutolea dhabihu ya kukushukuru na kuliita jina la BWANA. [18] Nitazitimiza nadhiri zangu kwa BWANA mbele za watu wake wote, [19] katika nyua za nyumba ya BWANA, katikati yako, ee Yerusalemu. Msifuni BWANA.