[1] Sio kwetu sisi, Ee BWANA, sio kwetu sisi, bali utukufu ni kwa jina lako, kwa sababu ya upendo na uaminifu wako. [2] Kwa nini mataifa waseme, “Yuko wapi Mungu wao?” [3] Mungu wetu yuko mbinguni, naye hufanya lolote limpendezalo. [4] Lakini sanamu zao ni za fedha na dhahabu, zilizotengenezwa kwa mikono ya wanadamu. [5] Zina vinywa, lakini haziwezi kusema, zina macho, lakini haziwezi kuona; [6] zina masikio, lakini haziwezi kusikia, zina pua, lakini haziwezi kunusa; [7] zina mikono, lakini haziwezi kupapasa, zina miguu, lakini haziwezi kutembea; wala koo zao haziwezi kutoa sauti. [8] Wale wanaozitengeneza watafanana nazo, vivyo hivyo wale wote wanaozitumainia. [9] Ee nyumba ya Israeli, mtumainini BWANA, yeye ni msaada na ngao yao. [10] Ee nyumba ya Aroni, mtumainini BWANA, yeye ni msaada na ngao yao. [11] Ninyi mnaomcha, mtumainini BWANA, yeye ni msaada na ngao yao. [12] BWANA anatukumbuka na atatubariki: ataibariki nyumba ya Israeli, ataibariki nyumba ya Aroni, [13] atawabariki wale wanaomcha BWANA, wadogo kwa wakubwa. [14] BWANA na awawezeshe kuongezeka, ninyi na watoto wenu. [15] Mbarikiwe na BWANA Muumba wa mbingu na dunia. [16] Mbingu zilizo juu sana ni mali ya BWANA, lakini dunia amempa mwanadamu. [17] Sio wafu wanaomsifu BWANA, wale washukao mahali pa kimya, [18] bali ni sisi tunaomtukuza BWANA, sasa na hata milele. Msifuni BWANA.