Yeremia 7:1-34 ONEN
[1] Hili ndilo neno lililomjia Yeremia kutoka kwa BWANA: [2] “Simama kwenye lango la nyumba ya BWANA, na huko upige mbiu ya ujumbe huu: “ ‘Sikieni neno la BWANA, enyi watu wote wa Yuda mliokuja kupitia malango haya ili kumwabudu BWANA. [3] Hili ndilo asemalo BWANA Mwenye Nguvu Zote, Mungu wa Israeli: Tengenezeni njia zenu na matendo yenu, nami nitawaacha mkae mahali hapa. [4] Msitumainie maneno ya udanganyifu na kusema, “Hili ni Hekalu la BWANA, Hekalu la BWANA, Hekalu la BWANA!” [5] Kama kweli mkibadili njia zenu na matendo yenu, mkatendeana haki kila mmoja na mwenzake, [6] kama msipomwonea mgeni, yatima wala mjane, na kumwaga damu isiyo na hatia mahali hapa, nanyi kama msipofuata miungu mingine kwa madhara yenu wenyewe, [7] ndipo nitawaacha mkae mahali hapa, katika nchi niliyowapa baba zenu milele na milele. [8] Lakini tazama, mnatumainia maneno ya udanganyifu yasiyo na maana. [9] “ ‘Je, mtaiba na kuua, mtazini na kuapa kwa uongo, na kufukiza uvumba kwa Baali, na kufuata miungu mingine ambayo hamkuijua, [10] kisha mje na kusimama mbele yangu katika nyumba hii inayoitwa kwa Jina langu, mkisema, “Tuko salama.” Salama kwa kufanya mambo haya yote ya kuchukiza? [11] Je, nyumba hii, iitwayo kwa Jina langu, imekuwa pango la wanyangʼanyi kwenu? Lakini nimekuwa nikiona yanayotendeka! asema BWANA. [12] “ ‘Nendeni sasa mahali pangu palipokuwa huko Shilo, mahali ambapo nilipafanya pa kwanza kuwa makao ya Jina langu, nanyi mwone lile nililopafanyia kwa ajili ya uovu wa watu wangu Israeli. [13] Mlipokuwa mnafanya yote haya, asema BWANA, nilisema nanyi tena na tena, lakini hamkusikiliza; niliwaita, lakini hamkujibu. [14] Kwa hiyo, nililolifanyia Shilo, nitalifanya sasa kwa nyumba hii iitwayo kwa Jina langu, Hekalu mnalolitumainia, mahali nilipowapa ninyi na baba zenu. [15] Nitawafukuza mbele yangu, kama nilivyowafanyia ndugu zenu, watu wa Efraimu.’ [16] “Kwa hiyo usiombe kwa ajili ya watu hawa, wala usinililie, na usifanye maombi kwa ajili yao; usinisihi, kwa sababu sitakusikiliza. [17] Je, huyaoni hayo wanayoyatenda katika miji ya Yuda na katika barabara za Yerusalemu? [18] Watoto wanakusanya kuni, baba zao wanawasha moto, na wanawake wanakanda unga na kuoka mikate kwa ajili ya Malkia wa Mbinguni. Wanamimina sadaka za vinywaji kwa miungu mingine ili kunikasirisha. [19] Lakini je, mimi ndiye wanayenikasirisha? asema BWANA. Je, hawajiumizi wenyewe na kujiaibisha? [20] “ ‘Kwa hiyo hivi ndivyo asemavyo BWANA Mwenyezi: Hasira yangu na ghadhabu yangu itamwagwa mahali hapa, juu ya mwanadamu na mnyama, juu ya miti ya shambani na juu ya matunda ya ardhini, nayo itaungua pasipo kuzimwa. [21] “ ‘Hivi ndivyo asemavyo BWANA Mwenye Nguvu Zote, Mungu wa Israeli: Endeleeni, ongezeni sadaka zenu za kuteketezwa juu ya dhabihu zenu nyingine, mle nyama hiyo wenyewe! [22] Kwa kuwa nilipowaleta baba zenu kutoka Misri na kusema nao, sikuwapa amri kuhusu sadaka za kuteketezwa na dhabihu tu, [23] lakini niliwapa amri hii nikisema: Nitiini mimi, nami nitakuwa Mungu wenu nanyi mtakuwa watu wangu. Enendeni katika njia zote ninazowaamuru ili mpate kufanikiwa. [24] Lakini hawakusikiliza wala kujali. Badala yake, walifuata ukaidi wa mioyo yao miovu. Walirudi nyuma badala ya kusonga mbele. [25] Tangu wakati ule baba zenu walipotoka Misri hadi sasa, siku baada ya siku, tena na tena nimewatumia watumishi wangu manabii. [26] Lakini hawakunisikiliza wala hawakujali. Walikuwa na shingo ngumu na kufanya maovu kuliko baba zao.’ [27] “Utakapowaambia haya yote, hawatakusikiliza; utakapowaita, hawatajibu. [28] Kwa hiyo waambie, ‘Hili ni taifa ambalo halimtii BWANA, Mungu wao, wala kukubali maonyo. Kweli imekufa, imetoweka midomoni mwao. [29] Nyoeni nywele zenu na kuzitupa, ombolezeni katika miinuko iliyo kame, kwa kuwa BWANA amekikataa na kukiacha kizazi hiki kilichomkasirisha. [30] “ ‘Watu wa Yuda wamefanya maovu machoni pangu, asema BWANA. Wameziweka sanamu zao za machukizo ndani ya nyumba iitwayo kwa Jina langu, na wameitia unajisi. [31] Wamejenga mahali pa juu pa kuabudia sanamu pa Tofethi kwenye Bonde la Ben-Hinomu ili kuwateketeza wana wao na binti zao kwenye moto, kitu ambacho sikuamuru, wala hakikuingia akilini mwangu. [32] Kwa hiyo mjihadhari, siku zinakuja, asema BWANA, wakati watu watakapokuwa hawapaiti Tofethi au Bonde la Ben-Hinomu, lakini watapaita Bonde la Machinjo, kwa sababu watawazika wafu huko Tofethi mpaka pasiwe tena nafasi. [33] Ndipo mizoga ya watu hawa itakuwa chakula cha ndege wa angani na wanyama wa nchi, wala hapatakuwepo na yeyote wa kuwafukuza. [34] Nitazikomesha sauti za shangwe na furaha, na sauti za bwana arusi na bibi arusi katikati ya miji ya Yuda na barabara za Yerusalemu, kwa sababu nchi itakuwa ukiwa.
