Yeremia 6:1-30 ONEN
[1] “Kimbieni kwa usalama wenu, enyi watu wa Benyamini! Kimbieni kutoka Yerusalemu! Pigeni tarumbeta katika Tekoa! Inueni ishara juu ya Beth-Hakeremu! Kwa kuwa maafa yanaonekana yakitoka kaskazini, na uharibifu wa kutisha. [2] Nitamwangamiza Binti Sayuni, aliye mzuri sana na mwororo. [3] Wachungaji pamoja na makundi yao watakuja dhidi yake; watapiga mahema yao kumzunguka, kila mmoja akichunga kundi lake mwenyewe.” [4] “Jiandaeni kwa vita dhidi yake! Inukeni tumshambulie mchana! Lakini, ole wetu, mchana unaisha, na vivuli vya jioni vinazidi kuwa virefu. [5] Kwa hiyo inukeni, tufanye mashambulizi usiku, na kuharibu ngome zake!” [6] Hivi ndivyo asemavyo BWANA Mwenye Nguvu Zote: “Kateni miti mjenge boma kuzunguka Yerusalemu. Mji huu ni lazima uadhibiwe, umejazwa na uonevu. [7] Kama vile kisima kinavyomwaga maji yake, ndivyo anavyomwaga uovu wake. Ukatili na maangamizi yasikika ndani yake, ugonjwa wake na majeraha yake viko mbele yangu daima. [8] Pokea onyo, ee Yerusalemu, la sivyo nitageukia mbali nawe na kuifanya nchi yako kuwa ukiwa, asiweze mtu kuishi ndani yake.” [9] Hivi ndivyo asemavyo BWANA Mwenye Nguvu Zote: “Wao na wayakusanye mabaki ya Israeli kwa uangalifu kama kwenye mzabibu; pitisha mkono wako kwenye matawi tena, kama yeye avunaye zabibu.” [10] Niseme na nani na kumpa onyo? Ni nani atakayenisikiliza mimi? Masikio yao yameziba, kwa hiyo hawawezi kusikia. Neno la BWANA ni chukizo kwao, hawalifurahii. [11] Lakini nimejaa ghadhabu ya BWANA, nami siwezi kuizuia. “Wamwagie watoto walioko barabarani, na juu ya vijana waume waliokusanyika; mume na mke watakumbwa pamoja ndani yake, hata nao wazee waliolemewa na miaka. [12] Nyumba zao zitapewa watu wengine, pamoja na mashamba yao na wake zao, nitakapounyoosha mkono wangu dhidi ya wale waishio katika nchi,” asema BWANA. [13] “Kuanzia aliye mdogo kabisa hadi aliye mkubwa kabisa, wote wana tamaa ya kupata faida zaidi; manabii na makuhani wanafanana, wote wanafanya udanganyifu. [14] Wanafunga majeraha ya watu wangu bila uangalifu. Wanasema, ‘Amani, amani,’ wakati hakuna amani. [15] Je, wanaona aibu kwa ajili ya tabia yao inayochukiza mno? Hapana, hawana aibu hata kidogo; hawajui hata kuona haya. Kwa hiyo wataanguka miongoni mwa hao walioanguka, watashushwa chini nitakapowaadhibu,” asema BWANA. [16] Hivi ndivyo asemavyo BWANA: “Simama kwenye njia panda utazame, ulizia mapito ya zamani, ulizia wapi ilipo njia nzuri, uifuate hiyo, nanyi mtapata raha nafsini mwenu. Lakini ninyi mlisema, ‘Hatutaipita hiyo.’ [17] Niliweka walinzi juu yenu na kusema, ‘Sikieni sauti ya tarumbeta!’ Lakini mkasema, ‘Hatutasikiliza.’ [18] Kwa hiyo sikilizeni, enyi mataifa, angalieni, enyi mashahidi, lile litakalowatokea. [19] Sikia, ee nchi: Ninaleta maafa juu ya watu hawa, matunda ya mipango yao, kwa sababu hawakusikiliza maneno yangu na wameikataa sheria yangu. [20] Unanifaa nini uvumba kutoka Sheba, au udi wa harufu nzuri kutoka nchi ya mbali? Sadaka zako za kuteketezwa hazikubaliki, dhabihu zako hazinifurahishi mimi.” [21] Kwa hiyo hivi ndivyo asemavyo BWANA: “Nitaweka vikwazo mbele ya watu hawa. Baba na wana wao watajikwaa juu yake, majirani na marafiki wataangamia.” [22] Hivi ndivyo asemavyo BWANA: “Tazama, jeshi linakuja kutoka nchi ya kaskazini, taifa kubwa linaamshwa kutoka miisho ya dunia. [23] Wamejifunga pinde na mkuki, ni wakatili na hawana huruma. Wanatoa sauti kama bahari inayonguruma wanapoendesha farasi zao. Wanakuja kama watu waliojipanga tayari kwa vita ili kukushambulia, ee Binti Sayuni.” [24] Tumesikia taarifa zao, nayo mikono yetu imelegea. Uchungu umetushika, maumivu kama ya mwanamke katika utungu wa kuzaa. [25] Usitoke kwenda mashambani au kutembea barabarani, kwa kuwa adui ana upanga, na kuna vitisho kila upande. [26] Enyi watu wangu, vaeni magunia mjivingirishe kwenye majivu, ombolezeni kwa kilio cha uchungu kama amliliaye mwana pekee, kwa maana ghafula mharabu atatujia. [27] “Nimekufanya wewe kuwa kitu cha kujaribu chuma, nao watu wangu kama mawe yenye madini, ili upate kuzijua na kuzijaribu njia zao. [28] Wote ni waasi sugu, wakienda huku na huko kusengenya. Wao ni shaba na chuma, wote wanatenda upotovu. [29] Mivuo inavuma kwa nguvu, kinachoungua kwa huo moto ni risasi, lakini pamoja na kusafisha kote huku ni bure; waovu hawaondolewi. [30] Wanaitwa fedha iliyokataliwa, kwa sababu BWANA amewakataa.”
