Waefeso 6:1-24 ONEN
[1] Enyi watoto, watiini wazazi wenu katika Bwana, kwa kuwa hili ni jema. [2] “Waheshimu baba yako na mama yako,” hii ndio amri ya kwanza yenye ahadi, [3] “upate baraka na uishi siku nyingi duniani.” [4] Ninyi akina baba, msiwachokoze watoto wenu, bali waleeni kwa nidhamu na mafundisho ya Bwana. [5] Ninyi watumwa, watiini hao walio mabwana zenu hapa duniani kwa heshima na kwa kutetemeka na kwa moyo mmoja, kama vile mnavyomtii Kristo. [6] Watiini, si tu wakati wakiwaona ili mpate upendeleo wao, bali mtumike kama watumwa wa Kristo, mkifanya mapenzi ya Mungu kwa moyo. [7] Tumikeni kwa moyo wote, kama vile mnamtumikia Bwana na si wanadamu. [8] Mkijua kwamba Bwana atampa kila mtu thawabu kwa lolote jema alilotenda, kama yeye ni mtumwa au ni mtu huru. [9] Nanyi mabwana, watendeeni watumwa wenu kwa jinsi iyo hiyo. Msiwatishe, kwa kuwa mnajua ya kwamba yeye aliye Bwana wenu na Bwana wao yuko mbinguni, naye hana upendeleo. [10] Hatimaye, mzidi kuwa hodari katika Bwana na katika uweza wa nguvu zake. [11] Vaeni silaha zote za Mungu ili kwamba mweze kuzipinga hila za ibilisi. [12] Kwa maana kushindana kwetu si juu ya nyama na damu, bali dhidi ya falme, mamlaka, dhidi ya wakuu wa giza na majeshi ya pepo wabaya katika ulimwengu wa roho. [13] Kwa hiyo vaeni silaha zote za Mungu ili mweze kushindana siku ya uovu itakapokuja nanyi mkiisha kufanya yote, simameni imara. [14] Kwa hiyo simameni imara mkiwa mmejifunga kweli kiunoni na kuvaa dirii ya haki kifuani, [15] nayo miguu yenu ifungiwe utayari tuupatao kwa Injili ya amani. [16] Zaidi ya haya yote, twaeni ngao ya imani, ambayo kwa hiyo mtaweza kuizima mishale yote yenye moto ya yule mwovu. [17] Vaeni chapeo ya wokovu na mchukue upanga wa Roho, ambao ni Neno la Mungu. [18] Mkiomba kwa Roho siku zote katika sala zote na maombi, mkikesha kila wakati mkiwaombea watakatifu wote. [19] Niombeeni na mimi pia, ili kila nifunguapo kinywa changu, nipewe maneno ya kusema, niweze kutangaza siri ya Injili kwa ujasiri, [20] ambayo mimi ni balozi wake katika vifungo. Ombeni ili nipate kuhubiri kwa ujasiri kama inipasavyo. [21] Tikiko, aliye ndugu mpendwa na mtumishi mwaminifu katika Bwana, atawaambia kila kitu, ili pia mpate kujua hali yangu na kile ninachofanya sasa. [22] Ninamtuma kwenu kwa ajili ya kusudi hili hasa, ili mpate kujua hali yetu, na awatie moyo. [23] Amani iwe kwa ndugu, na pendo pamoja na imani kutoka kwa Mungu Baba na Bwana Yesu Kristo. [24] Neema iwe na wote wampendao Bwana wetu Yesu Kristo kwa upendo wa dhati. Amen.
