Waefeso 5:1-33 ONEN
[1] Kwa hiyo, mfuateni Mungu kama watoto wapendwao, [2] mkiishi maisha ya upendo, kama vile Kristo alivyotupenda sisi akajitoa kwa ajili yetu kuwa sadaka yenye harufu nzuri na dhabihu kwa Mungu. [3] Lakini uasherati, usitajwe miongoni mwenu, wala uchafu wa aina yoyote, wala tamaa, kwa sababu mambo haya hayastahili miongoni mwa watakatifu. [4] Wala pasiwepo mazungumzo machafu ya aibu, au maneno ya upuzi au mzaha, ambayo hayafai, badala yake mshukuruni Mungu. [5] Kwa habari ya mambo haya mjue hakika kwamba: Msherati, wala mtu mwovu, wala mwenye tamaa mbaya, mtu kama huyo ni mwabudu sanamu, kamwe hataurithi Ufalme wa Kristo na wa Mungu. [6] Mtu yeyote na asiwadanganye kwa maneno matupu, kwa kuwa hasira ya Mungu huwaka kwa sababu ya mambo kama haya juu ya wale wasiomtii. [7] Kwa hiyo, msishirikiane nao. [8] Kwa maana zamani ninyi mlikuwa giza, lakini sasa ninyi ni nuru katika Bwana. Enendeni kama watoto wa nuru [9] (kwa kuwa tunda la nuru hupatikana katika wema wote, haki na kweli), [10] nanyi tafuteni yale yanayompendeza Bwana. [11] Msishiriki matendo ya giza yasiyofaa, bali yafichueni. [12] Kwa maana ni aibu hata kutaja mambo yale ambayo wasiotii wanayafanya sirini. [13] Lakini kila kitu kilichowekwa nuruni, huonekana, [14] kwa kuwa nuru ndiyo hufanya kila kitu kionekane. Hii ndiyo sababu imesemekana: “Amka, wewe uliyelala, ufufuke kutoka kwa wafu, naye Kristo atakuangazia.” [15] Kwa hiyo angalieni sana jinsi mnavyoenenda, si kama watu wasio na hekima, bali kama wenye hekima, [16] mkiukomboa wakati, kwa sababu nyakati hizi ni za uovu. [17] Kwa hiyo msiwe wajinga, bali mpate kujua nini mapenzi ya Bwana. [18] Pia msilewe kwa mvinyo, ambamo ndani yake mna upotovu, bali mjazwe Roho. [19] Msemezane ninyi kwa ninyi kwa zaburi, nyimbo na tenzi za rohoni, mkimwimbia na kumsifu Bwana mioyoni mwenu, [20] siku zote mkimshukuru Mungu Baba kwa kila jambo katika Jina la Bwana wetu Yesu Kristo. [21] Nyenyekeaneni ninyi kwa ninyi kwa heshima kwa ajili ya Kristo. [22] Ninyi wake, watiini waume zenu kama kumtii Bwana. [23] Kwa maana mume ni kichwa cha mkewe kama vile Kristo alivyo kichwa cha Kanisa, ambalo ni mwili wake, naye Kristo ni Mwokozi wake. [24] Basi, kama vile Kanisa linavyomtii Kristo, vivyo hivyo na wake nao imewapasa kuwatii waume zao kwa kila jambo. [25] Ninyi waume, wapendeni wake zenu, kama vile Kristo alivyolipenda Kanisa akajitoa kwa ajili yake [26] kusudi alifanye takatifu, akilitakasa kwa kuliosha kwa maji katika Neno lake, [27] apate kujiletea Kanisa tukufu lisilo na doa wala kunyanzi au waa lolote, bali takatifu na lisilo na hatia. [28] Vivyo hivyo imewapasa waume kuwapenda wake zao kama miili yao wenyewe. Ampendaye mkewe hujipenda mwenyewe. [29] Hakuna mtu anayeuchukia mwili wake mwenyewe, bali huulisha na kuutunza vizuri, kama Kristo anavyolitunza Kanisa lake. [30] Sisi tu viungo vya mwili wake. [31] “Kwa sababu hii, mwanaume atamwacha baba yake na mama yake, naye ataambatana na mkewe, na hao wawili watakuwa mwili mmoja.” [32] Siri hii ni kubwa, bali mimi nanena kuhusu Kristo na Kanisa. [33] Hata hivyo, kila mmoja wenu ampende mkewe kama anavyoipenda nafsi yake mwenyewe, naye mke lazima amheshimu mumewe.
