Mwanzo 4:1-26 ONEN
[1] Adamu akakutana kimwili na mkewe Eva, naye akapata mimba, akamzaa Kaini. Eva akasema, “Kwa msaada wa BWANA nimemzaa mwanaume.” [2] Baadaye akamzaa Abeli ndugu yake. Basi Abeli akawa mfugaji, na Kaini akawa mkulima. [3] Baada ya muda Kaini akaleta baadhi ya mazao ya shamba kama sadaka kwa BWANA. [4] Lakini Abeli akaleta fungu nono kutoka baadhi ya wazaliwa wa kwanza wa mifugo yake. BWANA akamkubali Abeli pamoja na sadaka yake, [5] lakini Mungu hakumkubali Kaini pamoja na sadaka yake. Kwa hiyo Kaini akakasirika sana, uso wake ukawa na huzuni. [6] Kisha BWANA akamwambia Kaini, “Kwa nini umekasirika? Kwa nini uso wako una huzuni? [7] Ukifanya lililo sawa, je, hutakubalika? Lakini usipofanya lililo sawa, dhambi inakuvizia mlangoni mwako, inakutamani wewe, lakini inakupasa uishinde.” [8] Basi Kaini akamwambia ndugu yake Abeli, “Twende shambani.” Walipokuwa shambani, Kaini akamshambulia Abeli ndugu yake, akamuua. [9] Kisha BWANA akamuuliza Kaini, “Ndugu yako Abeli yuko wapi?” Akamjibu, “Sijui, je, mimi ni mlinzi wa ndugu yangu?” [10] BWANA akasema, “Umefanya nini? Sikiliza! Damu ya ndugu yako inanililia mimi kutoka ardhini. [11] Sasa umelaaniwa na umehamishwa kutoka ardhi, ambayo imefungua kinywa chake na kupokea damu ya ndugu yako kutoka mkononi mwako. [12] Utakapoilima ardhi, haitakupa tena mazao yake. Utakuwa mtu wa kutangatanga duniani asiye na utulivu.” [13] Kaini akamwambia BWANA, “Adhabu yangu ni zaidi ya niwezavyo kustahimili. [14] Leo unanifukuza kutoka nchi, nami nitafichwa mbali na uwepo wako. Nitakuwa mtu wa kutangatanga asiyetulia duniani na yeyote anionaye ataniua.” [15] Lakini BWANA akamwambia, “La sivyo, ikiwa mtu yeyote atamuua Kaini atalipizwa kisasi mara saba zaidi.” Kisha BWANA akamwekea Kaini alama ili mtu yeyote ambaye angemwona asimuue. [16] Kwa hiyo Kaini akaondoka mbele za BWANA akaenda kuishi katika nchi ya Nodi, iliyoko mashariki ya Edeni. [17] Kaini akakutana kimwili na mkewe, naye akapata mimba na akamzaa Enoki. Wakati huo Kaini alikuwa anajenga mji, akauita Enoki jina la mtoto wake. [18] Enoki akamzaa Iradi, Iradi akamzaa Mehuyaeli, Mehuyaeli akamzaa Methushaeli, na Methushaeli akamzaa Lameki. [19] Lameki alioa wanawake wawili, mmoja aliitwa Ada, na mwingine Sila. [20] Ada akamzaa Yabali ambaye ni baba wa wale walioishi katika mahema na kufuga wanyama. [21] Kaka yake aliitwa Yubali, aliyekuwa baba wa wote wapigao zeze na filimbi. [22] Pia Sila alikuwa na mtoto wa kiume aliyeitwa Tubali-Kaini ambaye alifua vifaa vya aina mbalimbali vya shaba na chuma. Naama alikuwa dada wa Tubali-Kaini. [23] Lameki akawaambia wake zake, “Ada na Sila nisikilizeni mimi; wake wa Lameki sikieni maneno yangu. Nimemuua mtu kwa kunijeruhi, kijana mdogo kwa kuniumiza. [24] Kama Kaini atalipizwa kisasi mara saba, basi Lameki itakuwa mara sabini na saba.” [25] Adamu akakutana kimwili na mke wake tena, akamzaa mwana, akamwita Sethi, akisema, “Mungu amenijalia mwana mwingine badala ya Abeli, kwa kuwa Kaini alimuua.” [26] Naye Sethi akamzaa mwana, akamwita Enoshi. Wakati huo watu wakaanza kuliitia jina la BWANA.
