[1] Basi Sarai, mkewe Abramu, alikuwa hajamzalia watoto. Lakini alikuwa na mtumishi wa kike Mmisri jina lake Hagari, [2] hivyo Sarai akamwambia Abramu, “BWANA amenizuilia kupata watoto. Nenda, ukakutane kimwili na mtumishi wangu wa kike, huenda nitaweza kupata watoto kupitia kwake.” Abramu akakubaliana na lile Sarai alilosema. [3] Hivyo baada ya Abramu kuishi katika nchi ya Kanaani miaka kumi, Sarai akamchukua mtumishi wake wa kike wa Kimisri, Hagari na kumpa mumewe awe mke wake. [4] Akakutana kimwili na Hagari, naye akapata mimba. Hagari alipojua kuwa ana mimba, alianza kumdharau Sarai. [5] Ndipo Sarai akamwambia Abramu, “Unawajibika na manyanyaso ninayoyapata. Nilimweka mtumishi wangu mikononi mwako, sasa kwa vile anajua kwamba ana mimba, ananidharau mimi. BWANA na aamue kati yako na mimi.” [6] Abramu akamwambia, “Mtumishi wako yuko mikononi mwako. Mtendee lolote unalofikiri ni bora zaidi.” Ndipo Sarai akamtesa Hagari, hivyo akamtoroka. [7] Malaika wa BWANA akamkuta Hagari karibu na chemchemi huko jangwani; ilikuwa chemchemi ile iliyokuwa kando ya barabara iendayo Shuri. [8] Malaika akamwambia, “Hagari, mtumishi wa Sarai, umetokea wapi, na unakwenda wapi?” Akamjibu, “Ninamkimbia bibi yangu Sarai.” [9] Ndipo malaika wa BWANA akamwambia, “Rudi kwa bibi yako ukajishushe chini yake.” [10] Malaika akaendelea akasema, “Nitazidisha wazao wako, hivi kwamba watakuwa wengi mno wasiohesabika.” [11] Pia malaika wa BWANA akamwambia: “Wewe sasa una mimba nawe utamzaa mwana. Utamwita jina lake Ishmaeli, kwa sababu BWANA amesikia juu ya huzuni yako. [12] Atakuwa punda-mwitu katikati ya wanadamu, mkono wake utakuwa dhidi ya kila mtu na mkono wa kila mtu dhidi yake, naye ataishi kwa uhasama na ndugu zake wote.” [13] Hagari akampa BWANA aliyezungumza naye jina hili: “Wewe ndiwe Mungu unionaye mimi,” kwa maana alisema, “Sasa nimemwona yeye anayeniona mimi.” [14] Ndiyo sababu kisima kile kikaitwa Beer-Lahai-Roi, ambacho bado kipo huko hata leo kati ya Kadeshi na Beredi. [15] Hivyo Hagari akamzalia Abramu mwana, naye Abramu akamwita huyo mwana Hagari aliyemzalia, Ishmaeli. [16] Abramu alikuwa na umri wa miaka themanini na sita wakati Hagari alipomzalia Ishmaeli.