Mwanzo 15:1-21 ONEN

[1] Baada ya jambo hili, neno la BWANA likamjia Abramu katika maono: “Usiogope, Abramu. Mimi ni ngao yako, na thawabu yako kubwa sana.” [2] Lakini Abramu akasema, “Ee BWANA Mwenyezi, utanipa nini na mimi sina hata mtoto na atakayerithi nyumba yangu ni huyu Eliezeri Mdameski?” [3] Abramu akasema, “Hukunipa watoto, hivyo mtumishi katika nyumba yangu ndiye atakuwa mrithi wangu.” [4] Ndipo neno la BWANA lilipomjia: “Mtu huyu hatakuwa mrithi wako, bali mwana atakayetoka katika viuno vyako mwenyewe ndiye atakayekuwa mrithi wako.” [5] Akamtoa nje na kusema, “Tazama juu kuelekea mbinguni na uhesabu nyota, kama hakika utaweza kuzihesabu.” Ndipo akamwambia, “Hivyo ndivyo uzao wako utakavyokuwa.” [6] Abramu akamwamini BWANA, naye kwake hili likahesabiwa kuwa haki. [7] Pia akamwambia, “Mimi ndimi BWANA, niliyekutoa toka Uru ya Wakaldayo nikupe nchi hii uimiliki.” [8] Lakini Abramu akasema, “Ee BWANA Mwenyezi, nitawezaje kujua kwamba nitapata kuimiliki?” [9] Ndipo BWANA akamwambia, “Niletee mtamba wa ngʼombe, mbuzi na kondoo dume, kila mmoja wa miaka mitatu, pamoja na hua na kinda la njiwa.” [10] Abramu akamletea hivi vyote, akampasua kila mnyama vipande viwili, akavipanga kila kimoja kuelekea mwenzake, lakini hata hivyo ndege, hakuwapasua vipande viwili. [11] Kisha ndege walao nyama wakatua juu ya mizoga, lakini Abramu akawafukuza. [12] Wakati jua lilipokuwa linatua, Abramu akashikwa na usingizi mzito, giza nene na la kutisha likaja juu yake. [13] Kisha BWANA akamwambia, “Ujue hakika kwamba wazao wako watakuwa wageni kwenye nchi ambayo si yao, nao watafanywa watumwa na kuteswa kwa miaka mia nne. [14] Lakini nitaliadhibu taifa lile watakalolitumikia kama watumwa, na baadaye watatoka huko na mali nyingi. [15] Wewe, hata hivyo utakwenda kwa baba zako kwa amani na kuzikwa katika uzee mwema. [16] Katika kizazi cha nne wazao wako watarudi hapa, kwa maana dhambi ya Waamori bado haijafikia kipimo kilichojaa.” [17] Wakati jua lilipokuwa limezama na giza limeingia, tanuru la moshi na mwali wa moto unaowaka vikatokea na kupita kati ya vile vipande vya nyama. [18] Siku hiyo BWANA akafanya Agano na Abramu, na kumwambia, “Nitawapa wazao wako nchi hii, kuanzia Kijito cha Misri hadi mto ule mkubwa, Frati, [19] yaani nchi ya Wakeni, Wakenizi, Wakadmoni, [20] Wahiti, Waperizi, Warefai, [21] Waamori, Wakanaani, Wagirgashi na Wayebusi.”

About this translation

Life Bible app icon
Get the Life Bible app Read offline, sync highlights and notes, and study with your library on any device.