[1] “Njooni, ninyi nyote wenye kiu, njooni kwenye maji; nanyi ambao hamna fedha, njooni, nunueni na mle! Njooni, nunueni divai na maziwa bila fedha na bila gharama. [2] Kwa nini kutumia fedha kwa kitu ambacho si chakula, na kutaabikia kitu kisichoshibisha? Sikilizeni, nisikilizeni mimi na mle kilicho kizuri, nazo nafsi zenu zitafurahia utajiri wa unono. [3] Tegeni sikio mje kwangu, nisikieni mimi, ili nafsi zenu zipate kuishi. Nitafanya agano la milele nanyi, pendo la uaminifu nililomwahidi Daudi. [4] Tazama, nimemfanya kuwa shahidi wa mataifa, kiongozi na jemadari wa mataifa. [5] Hakika utaita mataifa usiyoyajua, nayo mataifa yale yasiyokujua yataharakisha kukujia, kwa sababu ya BWANA Mungu wako, yeye Aliye Mtakatifu wa Israeli, kwa maana amekutukuza.” [6] Mtafuteni BWANA maadamu anapatikana; mwiteni maadamu yu karibu. [7] Mtu mwovu na aiache njia yake, na mtu mbaya na ayaache mawazo yake. Yeye na amrudie BWANA, naye atamrehemu, arudi kwa Mungu wetu, kwa kuwa atamsamehe bure kabisa. [8] “Kwa kuwa mawazo yangu si mawazo yenu, wala njia zenu si njia zangu,” asema BWANA. [9] “Kama vile mbingu zilivyo juu kuliko dunia, ndivyo njia zangu zilivyo juu kuliko njia zenu na mawazo yangu kuliko mawazo yenu. [10] Kama vile mvua na theluji ishukavyo kutoka mbinguni, nayo hairudi tena huko bila kunywesha dunia na kuichipusha na kuistawisha, hivyo hutoa mbegu kwa mpanzi na mkate kwa mlaji, [11] ndivyo lilivyo neno langu lile litokalo kinywani mwangu: Halitanirudia tupu, bali litatimiliza lile nililokusudia na litafanikiwa katika kusudi lile nililolituma. [12] Mtatoka nje kwa furaha na kuongozwa kwa amani; milima na vilima vitapaza sauti kwa nyimbo mbele yenu, nayo miti yote ya shambani itapiga makofi. [13] Badala ya kichaka cha miiba itaota miti ya misunobari, na badala ya michongoma utaota mhadasi. Hili litakuwa jambo la kumpatia BWANA jina, kwa ajili ya ishara ya milele, ambayo haitaharibiwa.”