Isaya 54:1-17 ONEN
[1] “Imba, ewe mwanamke tasa, wewe ambaye kamwe hukuzaa mtoto; paza sauti kwa kuimba, piga kelele kwa furaha, wewe ambaye kamwe hukupata utungu; kwa sababu watoto wa mwanamke aliyeachwa ukiwa ni wengi kuliko wa mwanamke mwenye mume,” asema BWANA. [2] “Panua mahali pa hema lako, tandaza mapazia ya hema lako uyaeneze mbali, wala usiyazuie; ongeza urefu wa kamba zako, imarisha vigingi vyako. [3] Kwa maana utaenea upande wa kuume na upande wa kushoto; wazao wako watayamiliki mataifa na kukaa katika miji yao iliyoachwa ukiwa. [4] “Usiogope, wewe hutaaibika. Usiogope aibu, wewe hutaaibishwa. Wewe utasahau aibu ya ujana wako, wala hutakumbuka tena mashutumu ya ujane wako. [5] Kwa maana Muumba wako ndiye mume wako, BWANA Mwenye Nguvu Zote ndilo jina lake, yeye Aliye Mtakatifu wa Israeli ni Mkombozi wako, yeye anaitwa Mungu wa dunia yote. [6] BWANA atakuita urudi kana kwamba ulikuwa mke aliyeachwa na kuhuzunishwa rohoni; kama mke aliyeolewa bado angali kijana na kukataliwa,” asema Mungu wako. [7] “Kwa kitambo kidogo nilikuacha, lakini kwa huruma nyingi nitakurudisha. [8] Katika ukali wa hasira nilikuficha uso wangu kwa kitambo, lakini kwa fadhili za milele nitakuwa na huruma juu yako,” asema BWANA Mkombozi wako. [9] “Kwangu mimi jambo hili ni kama siku za Noa, nilipoapa kuwa maji ya Noa kamwe hayatafunika tena dunia. Hivyo sasa nimeapa sitawakasirikia ninyi, kamwe sitawakemea tena. [10] Ijapotikisika milima, na vilima viondolewe, hata hivyo upendo wangu usiokoma kwenu hautatikisika, wala agano langu la amani halitaondolewa,” asema BWANA, mwenye huruma juu yenu. [11] “Ewe mji uliyeteswa, uliyepigwa kwa dhoruba na usiyetulizwa, nitakujenga kwa almasi, nitaweka misingi yako kwa yakuti samawi. [12] Nitafanya minara yako ya akiki, malango yako kwa vito vingʼaavyo, nazo kuta zako zote za vito vya thamani. [13] Watoto wako wote watafundishwa na BWANA, nayo amani ya watoto wako itakuwa kuu. [14] Kwa haki utathibitika: Kuonewa kutakuwa mbali nawe; hutaogopa chochote. Hofu itakuwa mbali nawe; haitakukaribia wewe. [15] Kama mtu yeyote akikushambulia, haitakuwa kwa ruhusa yangu; yeyote akushambuliaye atajisalimisha kwako. [16] “Tazama, ni mimi niliyemuumba mhunzi, yeye afukutaye makaa kuwa moto, na kutengeneza silaha inayofaa kwa kazi yake. Tena ni mimi niliyemwambia mharabu kufanya uharibifu mwingi. [17] Hakuna silaha itakayofanyizwa dhidi yako itakayofanikiwa, nawe utauthibitisha kuwa mwongo kila ulimi utakaokushtaki. Huu ndio urithi wa watumishi wa BWANA na hii ndiyo haki yao itokayo kwangu,” asema BWANA.
