Isaya 26:1-21 ONEN
[1] Katika siku ile, wimbo huu utaimbwa katika nchi ya Yuda: Tuna mji ulio na nguvu, Mungu huufanya wokovu kuwa kuta zake na maboma yake. [2] Fungua malango ili taifa lenye haki lipate kuingia, taifa lile lidumishalo imani. [3] Utamlinda katika amani kamilifu yeye ambaye moyo wake ni thabiti kwa sababu anakutumaini wewe. [4] Mtumaini BWANA milele, kwa kuwa BWANA, BWANA, ni Mwamba wa milele. [5] Huwashusha wale wajikwezao, huushusha chini mji wenye kiburi, huushusha hadi ardhini na kuutupa chini mavumbini. [6] Miguu huukanyaga chini, miguu ya hao walioonewa, hatua za hao maskini. [7] Mapito ya wenye haki yamenyooka. Ewe uliye Mwenye Haki, waisawazisha njia ya mtu mnyofu. [8] Naam, BWANA, tukienenda katika sheria zako, twakungojea wewe, jina lako na sifa zako ndizo shauku za mioyo yetu. [9] Nafsi yangu yakutamani wakati wa usiku, wakati wa asubuhi roho yangu yakuonea shauku. Wakati hukumu zako zinapokuja juu ya dunia, watu wa ulimwengu hujifunza haki. [10] Ingawa neema yaonyeshwa kwa waovu, hawajifunzi haki, hata katika nchi ya unyofu huendelea kutenda mabaya wala hawazingatii utukufu wa BWANA. [11] Ee BWANA, mkono wako umeinuliwa juu, lakini hawauoni. Wao na waone wivu wako kwa ajili ya watu wako tena waaibishwe, moto uliowekwa akiba kwa ajili ya adui zako na uwateketeze. [12] BWANA, unaamuru amani kwa ajili yetu, yale yote tuliyoweza kuyakamilisha ni wewe uliyetenda kwa ajili yetu. [13] Ee BWANA, Mungu wetu, mabwana wengine zaidi ya wewe wametutawala, lakini jina lako pekee ndilo tunaloliheshimu. [14] Wao sasa wamekufa, wala hawako tena hai, roho za waliokufa hazitarudi tena. Uliwaadhibu na kuwaangamiza, umefuta kumbukumbu lao lote. [15] Umeliongeza hilo taifa, Ee BWANA, umeliongeza hilo taifa. Umejipatia utukufu kwa ajili yako mwenyewe, umepanua mipaka yote ya nchi. [16] BWANA, walikujia katika taabu yao, wewe ulipowarudi, waliweza kuomba kwa kunongʼona tu. [17] Kama mwanamke mwenye mimba aliyekaribia kuzaa anavyogaagaa na kulia kwa ajili ya maumivu yake, ndivyo tulivyokuwa mbele zako, Ee BWANA. [18] Tulikuwa na mimba, tuligaagaa kwa maumivu, lakini tulizaa upepo. Hatukuleta wokovu duniani, hatujazaa watu katika ulimwengu huu. [19] Lakini wafu wenu wataishi, nayo miili yao itafufuka. Ninyi mnaokaa katika mavumbi, amkeni mkapige kelele kwa furaha. Umande wenu ni kama umande wa asubuhi, dunia itawazaa wafu wake. [20] Nendeni, watu wangu, ingieni vyumbani mwenu na mfunge milango nyuma yenu, jificheni kwa kitambo kidogo mpaka ghadhabu yake ipite. [21] Tazama, BWANA anakuja kutoka makao yake ili kuwaadhibu watu wa dunia kwa ajili ya dhambi zao. Dunia itadhihirisha umwagaji damu juu yake, wala haitaendelea kuwaficha watu wake waliouawa.
