[1] Ee BWANA, wewe ni Mungu wangu, nitakutukuza na kulisifu jina lako, kwa maana katika ukamilifu wa uaminifu umetenda mambo ya ajabu, mambo yaliyokusudiwa tangu zamani. [2] Umeufanya mji kuwa lundo la kifusi, mji wenye ngome kuwa magofu, ngome imara ya wageni kuwa si mji tena, wala hautajengwa tena kamwe. [3] Kwa hiyo mataifa yenye nguvu yatakuheshimu, miji ya mataifa katili itakuheshimu wewe. [4] Umekuwa kimbilio la watu maskini, kimbilio la mhitaji katika taabu yake, hifadhi wakati wa dhoruba na kivuli wakati wa hari. Kwa maana pumzi ya wakatili ni kama dhoruba ipigayo ukuta [5] na kama joto la jangwani. Wewe wanyamazisha makelele ya wageni; kama vile hari ipunguzwavyo na kivuli cha wingu, ndivyo wimbo wa wakatili unyamazishwavyo. [6] Juu ya mlima huu BWANA Mwenye Nguvu Zote ataandaa karamu ya vinono kwa mataifa yote, karamu ya mvinyo wa zamani, nyama nzuri sana na divai zilizo bora sana. [7] Juu ya mlima huu ataharibu sitara ihifadhiyo mataifa yote, kile kifuniko kifunikacho mataifa yote, [8] yeye atameza mauti milele. BWANA Mwenyezi atafuta machozi katika nyuso zote; ataondoa aibu ya watu wake duniani kote. BWANA amesema hili. [9] Katika siku ile watasema, “Hakika huyu ndiye Mungu wetu; tulimtumaini, naye akatuokoa. Huyu ndiye BWANA, tuliyemtumaini; sisi tushangilie na kufurahia katika wokovu wake.” [10] Mkono wa BWANA utatulia juu ya mlima huu, bali Moabu atakanyagwa chini kama majani makavu yakanyagwavyo kwenye shimo la mbolea. [11] Watakunjua mikono yao katikati yake, kama vile mwogeleaji akunjuavyo mikono yake ili aogelee. Mungu atashusha kiburi chao licha ya ujanja wa mikono yao. [12] Atabomoa kuta ndefu za maboma yako na kuziangusha chini, atazishusha chini ardhini, mpaka mavumbini kabisa.