[1] “Njooni, tumrudie BWANA. Ameturarua vipande vipande lakini atatuponya; ametujeruhi lakini atatufunga majeraha yetu. [2] Baada ya siku mbili atatufufua; katika siku ya tatu atatuinua, ili tuweze kuishi mbele zake. [3] Tumkubali BWANA, tukaze kumkubali yeye. Kutokea kwake ni hakika kama vile kuchomoza kwa jua; atatujia kama mvua za masika, kama vile mvua za vuli ziinyweshavyo nchi.” [4] “Nifanye nini nawe, Efraimu? Nifanye nini nawe, Yuda? Upendo wako ni kama ukungu wa asubuhi, kama umande wa alfajiri utowekao. [5] Kwa hiyo ninawakata ninyi vipande vipande kwa kutumia manabii wangu; nimewaua ninyi kwa maneno ya kinywa changu, hukumu zangu zinawaka kama umeme juu yenu. [6] Kwa maana nataka rehema, wala si dhabihu, kumkubali Mungu zaidi kuliko sadaka za kuteketezwa. [7] Wamevunja Agano kama Adamu: huko hawakuwa waaminifu kwangu. [8] Gileadi ni mji wenye watu waovu, umetiwa madoa kwa nyayo za damu. [9] Kama wanyangʼanyi wamviziavyo mtu, ndivyo magenge ya makuhani wafanyavyo; wanaulia watu kwenye njia iendayo Shekemu, wakifanya uhalifu wa aibu. [10] Nimeona jambo la kutisha katika nyumba ya Israeli. Huko Efraimu amejitolea kwa ukahaba na Israeli amenajisika. [11] “Pia kwa ajili yako, Yuda, mavuno yameamriwa. “Wakati wowote ningerejesha neema ya watu wangu,