[1] “Sikieni hili, enyi makuhani! Kuweni wasikivu, enyi Waisraeli! Sikieni, ee nyumba ya mfalme! Hukumu hii ni dhidi yenu: Mmekuwa mtego huko Mispa, wavu uliotandwa juu ya Tabori. [2] Waasi wamezidisha sana mauaji. Mimi nitawatiisha wote. [3] Ninajua yote kuhusu Efraimu, Israeli hukufichika kwangu. Efraimu, sasa umegeukia ukahaba, Israeli amenajisika. [4] “Matendo yao hayawaachii kurudi kwa Mungu wao. Roho ya ukahaba imo ndani ya mioyo yao, hawamkubali BWANA. [5] Kiburi cha Israeli kinashuhudia dhidi yao; Waisraeli, hata Efraimu, wanajikwaa katika dhambi zao; pia Yuda atajikwaa pamoja nao. [6] Wakati wanapokwenda na makundi yao ya kondoo na ngʼombe kumtafuta BWANA, hawatampata; yeye amejiondoa kutoka kwao. [7] Wao si waaminifu kwa BWANA; wamezaa watoto haramu. Sasa sikukuu zao za Mwandamo wa Mwezi zitawaangamiza wao pamoja na mashamba yao. [8] “Pigeni tarumbeta huko Gibea, baragumu huko Rama. Paza kilio cha vita huko Beth-Aveni, ongoza, ee Benyamini. [9] Efraimu ataachwa ukiwa katika siku ya kuadhibiwa. Miongoni mwa makabila ya Israeli ninatangaza lile ambalo halina budi kutukia. [10] Viongozi wa Yuda ni kama wale wanaosogeza mawe ya mpaka. Nitamwaga ghadhabu yangu juu yao kama mafuriko ya maji. [11] Efraimu ameonewa, amekanyagwa katika hukumu kwa kuwa amekusudia kufuatia sanamu. [12] Mimi ni kama nondo kwa Efraimu, na kama uozo kwa watu wa Yuda. [13] “Wakati Efraimu alipoona ugonjwa wake, naye Yuda vidonda vyake, ndipo Efraimu alipogeukia Ashuru, na kuomba msaada kwa mfalme mkuu. Lakini hawezi kukuponya, wala hawezi kukuponya vidonda vyako. [14] Kwa maana nitakuwa kama simba kwa Efraimu, kama simba mkubwa kwa Yuda. Nitawararua vipande vipande na kuondoka; nitawachukua mbali, na hakuna wa kuwaokoa. [15] Kisha nitarudi mahali pangu mpaka watakapokubali kosa lao. Nao watautafuta uso wangu; katika taabu yao watanitafuta kwa bidii.”