Hesabu 13:1-33 ONEN
[1] BWANA akamwambia Mose, [2] “Watume baadhi ya watu wakaipeleleze nchi ya Kanaani, ambayo ninawapa Waisraeli. Kutoka kwa kila kabila la baba zao, tuma mmoja wa viongozi wao.” [3] Hivyo kwa agizo la BWANA Mose akawatuma kutoka Jangwa la Parani. Wote walikuwa viongozi wa Waisraeli. [4] Haya ndiyo majina yao: kutoka kabila la Reubeni, Shamua mwana wa Zakuri; [5] kutoka kabila la Simeoni, Shafati mwana wa Hori; [6] kutoka kabila la Yuda, Kalebu mwana wa Yefune; [7] kutoka kabila la Isakari, Igali mwana wa Yosefu; [8] kutoka kabila la Efraimu, Hoshea mwana wa Nuni; [9] kutoka kabila la Benyamini, Palti mwana wa Rafu; [10] kutoka kabila la Zabuloni, Gadieli mwana wa Sodi, [11] kutoka kabila la Manase (kabila la Yosefu), Gadi mwana wa Susi; [12] kutoka kabila la Dani, Amieli mwana wa Gemali; [13] kutoka kabila la Asheri, Sethuri mwana wa Mikaeli; [14] kutoka kabila la Naftali, Nabi mwana wa Wofsi; [15] kutoka kabila la Gadi, Geueli mwana wa Maki. [16] Haya ndiyo majina ya watu ambao Mose aliwatuma kuipeleleza nchi. (Mose akampa Hoshea mwana wa Nuni jina Yoshua.) [17] Mose alipowatuma wakaipeleleze Kanaani, alisema, “Pandeni kupitia Negebu, mwende mpaka nchi ya vilima. [18] Mwone nchi ni ya namna gani, na kama watu waishio humo wana nguvu au ni wadhaifu, iwapo ni wachache au wengi. [19] Wanaishi katika nchi ya namna gani? Je, ni nzuri au mbaya? Wanaishi katika miji ya namna gani? Je, haina kuta au ngome? [20] Ardhi iko aje? Ina rutuba au la? Je, kuna miti ndani yake au la? Jitahidini kadiri mwezavyo kuleta baadhi ya matunda ya nchi.” (Ulikuwa msimu wa kuiva zabibu za kwanza.) [21] Hivyo wakapanda na kuipeleleza nchi kutoka Jangwa la Sini hadi Rehobu, kuelekea Lebo-Hamathi. [22] Wakapanda kupitia Negebu hadi wakafika Hebroni, mahali ambapo Ahimani, Sheshai na Talmai, wazao wa Anaki, waliishi. (Hebroni ulikuwa umejengwa miaka saba kabla ya mji wa Soani ulioko Misri.) [23] Walipofika katika Bonde la Eshkoli, walivunja tawi lililokuwa na kishada kimoja cha zabibu. Wawili wao wakalichukua lile tawi kwenye mti, pamoja na komamanga na tini. [24] Eneo lile likaitwa Bonde la Eshkoli kwa sababu ya kile kishada cha zabibu ambacho Waisraeli walikikata huko. [25] Mwishoni mwa siku arobaini wakarudi kutoka kuipeleleza nchi. [26] Wakarudi kwa Mose, Aroni na jumuiya yote ya Waisraeli huko Kadeshi kwenye Jangwa la Parani. Hapo ndipo walipotoa habari kwao na kwa kusanyiko lote na kuwaonyesha matunda ya hiyo nchi. [27] Wakampa Mose taarifa hii: “Tuliingia katika nchi uliyotutuma, nayo inatiririka maziwa na asali! Hili hapa tunda lake. [28] Lakini watu wanaoishi huko ni wenye nguvu, na miji yao ina ngome na ni mikubwa sana. Huko tuliona hata wazao wa Anaki. [29] Waamaleki wanaishi Negebu; Wahiti, Wayebusi na Waamori wanaishi katika nchi ya vilima; nao Wakanaani wanaishi karibu na bahari na kando ya Yordani.” [30] Kisha Kalebu akawanyamazisha watu mbele ya Mose na kusema, “Imetupasa kupanda na kuimiliki nchi, kwa maana hakika tunaweza kufanya hivyo.” [31] Lakini watu waliokuwa wamepanda pamoja naye wakasema, “Hatuwezi kuwashambulia wale watu; wana nguvu kutuliko sisi.” [32] Wakaeneza taarifa mbaya miongoni mwa Waisraeli kuhusu nchi waliyoipeleleza. Wakasema, “Nchi tuliyoipeleleza hula watu waishio ndani yake. Watu wote tuliowaona huko ni majitu. [33] Tuliwaona Wanefili huko (wazao wa Anaki wanatokana na Wanefili.) Tulijiona kama panzi machoni petu wenyewe, nao ndivyo walivyotuona.”
