[1] Miriamu na Aroni walianza kuzungumza dhidi ya Mose kwa sababu ya mke wake Mkushi, kwa kuwa alikuwa ameoa Mkushi. [2] Waliuliza, “Je, BWANA amesema kupitia Mose peke yake? Je, hajasema kutupitia sisi pia?” Naye BWANA akasikia hili. [3] (Basi Mose alikuwa mtu mnyenyekevu sana, mnyenyekevu kuliko mtu mwingine yeyote katika uso wa dunia.) [4] Ghafula BWANA akawaambia Mose, Aroni na Miriamu, “Njooni katika Hema la Kukutania, ninyi nyote watatu.” Kwa hiyo wote watatu wakaenda. [5] Kisha BWANA akashuka katika nguzo ya wingu, akasimama kwenye ingilio la Hema, akawaita Aroni na Miriamu. Wakati wote wawili waliposogea mbele, [6] BWANA akasema, “Sikilizeni maneno yangu: “Akiwapo nabii wa BWANA miongoni mwenu, nitajifunua kwake kwa maono, nitanena naye katika ndoto. [7] Lakini sivyo kwa mtumishi wangu Mose; yeye ni mwaminifu katika nyumba yangu yote. [8] Kwake nitanena naye uso kwa uso, waziwazi wala si kwa mafumbo; yeye ataona umbo la BWANA. Kwa nini basi ninyi hamkuogopa kuzungumza kinyume cha mtumishi wangu Mose?” [9] Hasira ya BWANA ikawaka dhidi yao, akawaacha. [10] Wakati hilo wingu liliinuka kutoka juu ya Hema, Miriamu akawa tayari ana ukoma, mweupe kama theluji. Aroni akamgeukia, akaona ana ukoma. [11] Kisha Aroni akamwambia Mose, “Tafadhali, bwana wangu, usituhesabie dhambi hii ambayo tumeifanya kwa upumbavu. [12] Usimwache awe kama mtoto mchanga aliyezaliwa akiwa mfu, ambaye nusu ya mwili wake imeharibika hapo atokapo katika tumbo la mama yake.” [13] Hivyo Mose akamlilia BWANA akisema, “Ee Mungu, nakuomba umponye!” [14] BWANA akamjibu Mose, “Je, kama baba yake angemtemea usoni, asingeona aibu kwa siku saba? Mfungie nje ya kambi kwa siku saba; baada ya hapo anaweza kurudishwa kambini.” [15] Kwa hiyo Miriamu akafungiwa nje ya kambi kwa siku saba, nao watu hawakuendelea na safari mpaka aliporudishwa kambini. [16] Baada ya hayo, watu waliondoka Haserothi, wakapiga kambi katika Jangwa la Parani.