[1] Sala ya nabii Habakuki iliyoimbwa kwa shigionothi. [2] BWANA, nimezisikia sifa zako; nami naogopa kwa matendo yako, Ee BWANA. Fufua kazi yako katikati ya miaka, katikati ya miaka tangaza habari yako; katika ghadhabu kumbuka rehema. [3] Mungu alitoka Temani, yeye Aliye Mtakatifu kutoka Mlima Parani. Utukufu wake ulifunika mbingu, na sifa zake zikaifunika dunia. [4] Mngʼao wake ulikuwa kama jua lichomozalo; mionzi ilimulika kutoka mkononi mwake, ambako nguvu zake zilifichwa. [5] Tauni ilimtangulia; maradhi ya kuambukiza yalifuata nyayo zake. [6] Alisimama, akaitikisa dunia; alitazama, na kuyafanya mataifa yatetemeke. Milima ya zamani iligeuka mavumbi na vilima vilivyozeeka vikaanguka. Njia zake ni za milele. [7] Niliona watu wa Kushani katika dhiki, na makazi ya Midiani katika maumivu makali. [8] Ee BWANA, uliikasirikia mito? Je, ghadhabu yako ilikuwa dhidi ya vijito? Je, ulighadhibikia bahari ulipoendesha farasi wako na magari yako ya ushindi? [9] Uliufunua upinde wako na kuita mishale mingi. Uliigawa dunia kwa mito; [10] milima ilikuona ikatetemeka. Mafuriko ya maji yakapita huko; vilindi vilinguruma na kuinua mawimbi yake juu. [11] Jua na mwezi vilisimama kimya mbinguni katika mngʼao wa mishale yako inayoruka, na katika mngʼao wa mkuki wako umeremetao. [12] Kwa ghadhabu ulipita juu ya dunia, na katika hasira ulikanyaga mataifa. [13] Ulikuja kuwaokoa watu wako, kumwokoa uliyemtia mafuta. Ulimponda kiongozi wa nchi ya uovu, ukamvua toka kichwani hadi wayo. [14] Kwa mkuki wake mwenyewe ulitoboa kichwa chake wakati mashujaa wake walifurika nje kwa kishindo kututawanya, wakifurahi kama walio karibu kutafuna wale wanyonge waliokuwa mafichoni. [15] Ulikanyaga bahari kwa farasi wako, ukisukasuka maji makuu. [16] Nilisikia na moyo wangu ukagonga kwa nguvu, midomo yangu ikatetemeka kwa hofu niliposikia sauti; uchakavu ukanyemelea mifupa yangu, na miguu yangu ikatetemeka. Hata hivyo nitasubiri kwa uvumilivu siku ya maafa kuyajilia mataifa yaliyotuvamia. [17] Ingawa mtini hauchanui maua na hakuna zabibu juu ya mizabibu, ingawaje mzeituni hauzai, na hata mashamba hayatoi chakula, iwapo hakuna kondoo katika banda, wala ngʼombe katika zizi, [18] hata hivyo nitashangilia katika BWANA, nitamfurahia Mungu Mwokozi wangu. [19] BWANA Mwenyezi ni nguvu yangu; huifanya miguu yangu kama miguu ya ayala, huniwezesha kupita juu ya vilima. Kwa kiongozi wa uimbaji. Kwa vinanda vyangu vya nyuzi.