Habakuki 2:1-20 ONEN
[1] Nitasimama katika zamu yangu, na kujiweka mwenyewe juu ya maboma; nitatazama nione atakaloniambia, na ni jibu gani nitakalotoa kuhusu lalamiko hili. [2] Kisha BWANA akajibu: “Andika ufunuo huu, na ukaufanye wazi juu ya vibao, ili mpiga mbiu akimbie nao. [3] Kwa kuwa ufunuo huu unasubiri wakati uliokubalika; unazungumzia mambo ya mwisho, na kamwe hautakosea. Iwapo utakawia, wewe usubiri; kwa hakika utakuja na hautachelewa. [4] “Tazama, amejaa majivuno; anavyovitamani si vya unyofu: lakini mwenye haki ataishi kwa imani yake: [5] hakika mvinyo humsaliti; ni mwenye kiburi na hana amani. Kwa sababu ni mlafi kama kuzimu na kama kifo kamwe hatosheki; anajikusanyia mataifa yote na kuchukua watu wote mateka. [6] “Je, watu wote hawatamsuta kwa dhihaka na kumbeza, wakisema, “ ‘Ole wake yeye akusanyaye bidhaa zilizoibwa na kujifanyia utajiri kwa kutoza kwa nguvu! Ataendelea hivi kwa muda gani?’ [7] Je, wadai wako hawatainuka ghafula? Je, hawataamka na kukufanya utetemeke? Kisha utakuwa mhanga kwao. [8] Kwa kuwa umeteka nyara mataifa mengi, watu waliobaki watakuteka nyara wewe. Kwa kuwa umemwaga damu ya mtu; umeharibu nchi na miji, na kila mmoja ndani yake. [9] “Ole wake yeye ajengaye milki yake kwa mapato ya udhalimu, awekaye kiota chake juu, ili kukimbia makucha ya uharibifu! [10] Umefanya shauri la maangamizi ya watu wengi, ukiaibisha nyumba yako mwenyewe, na kupotewa na maisha yako. [11] Mawe ya kuta yatapiga kelele, na mihimili ya kazi ya mbao itarudisha mwangwi wake. [12] “Ole wake yeye ajengaye mji kwa kumwaga damu na kuusimamisha mji kwa uhalifu! [13] Je, BWANA Mwenye Nguvu Zote hakuonyesha kwamba kazi ya wanadamu ni mafuta tu kwa ajili ya moto, na kwamba mataifa yanajichosha bure? [14] Kwa kuwa dunia itajazwa na maarifa ya utukufu wa BWANA, kama maji yaifunikavyo bahari. [15] “Ole wake yeye awapaye jirani zake kileo, akiimimina kutoka kwenye kiriba cha mvinyo mpaka wamelewa, ili apate kutazama miili yao iliyo uchi. [16] Utajazwa na aibu badala ya utukufu. Sasa ni zamu yako! Kunywa na ujifunue! Kikombe kutoka kwenye mkono wa kuume wa BWANA kinakujia, na aibu itafunika utukufu wako. [17] Ukatili ulioifanyia Lebanoni utakufunika, na uharibifu uliowafanyia wanyama utakutisha. Kwa sababu umemwaga damu ya mtu; umeharibu nchi na miji na kila mmoja aliyeko ndani yake. [18] “Sanamu ina thamani gani, kwani mwanadamu ndiye alichonga? Ama kinyago kinachofundisha uongo? Kwa kuwa yeye aliyekitengeneza hutegemea kazi ya mikono yake mwenyewe; hutengeneza sanamu zisizoweza kuzungumza. [19] Ole wake yeye auambiaye mti, ‘Uwe hai!’ Ama asemaye na jiwe lisilo na uhai, ‘Amka!’ Je, linaweza kuongoza? Limefunikwa kwa dhahabu na fedha; hakuna pumzi ndani yake. [20] Lakini BWANA yuko katika Hekalu lake takatifu; dunia yote na inyamaze mbele yake.”
