2 Nyakati 11:1-23 ONEN
[1] Ikawa Rehoboamu alipofika Yerusalemu, akakusanya nyumba ya Yuda na ya Benyamini, wanaume wapiganaji 180,000, kufanya vita dhidi ya nyumba ya Israeli na kuurudisha tena ufalme kwa Rehoboamu mwana wa Solomoni. [2] Lakini neno hili la BWANA likamjia Shemaya mtu wa Mungu: [3] “Mwambie Rehoboamu mwana wa Solomoni mfalme wa Yuda, na Israeli wote walioko Yuda na Benyamini, [4] ‘Hili ndilo asemalo BWANA: Msipande kupigana dhidi ya ndugu zenu. Nendeni nyumbani, kila mmoja wenu, kwa kuwa hili nimelitenda mimi.’ ” Kwa hiyo wakalitii neno la BWANA na wakaacha kwenda kupigana dhidi ya Yeroboamu. [5] Rehoboamu akaishi Yerusalemu akajenga miji yenye ngome katika Yuda: [6] Akajenga Bethlehemu, Etamu, Tekoa, [7] Beth-Suri, Soko, Adulamu, [8] Gathi, Maresha, Zifu, [9] Adoraimu, Lakishi, Azeka, [10] Sora, Aiyaloni na Hebroni. Hii ndiyo iliyokuwa miji iliyojengewa ngome katika Yuda na Benyamini. [11] Akaimarisha ulinzi wake na kuweka majemadari ndani yake, pamoja na ghala za mahitaji ya vyakula, mafuta ya zeituni na divai. [12] Akaweka ngao na mikuki katika miji na kuifanya iwe imara sana. Kwa hiyo Yuda na Benyamini zikawa zake. [13] Makuhani na Walawi kutoka sehemu zote za Israeli wakawa upande wake. [14] Pia Walawi wakaacha maeneo yao ya malisho na mali zao, wakaja Yuda na Yerusalemu kwa sababu Yeroboamu na wanawe walikuwa wamewakataa wasiwe makuhani wa BWANA. [15] Naye akawa amechagua makuhani wake mwenyewe kwa ajili ya mahali pa juu pa kuabudia sanamu za mbuzi na za ndama ambazo alikuwa ametengeneza. [16] Wale waliotoka katika kila kabila la Israeli ambao walielekeza mioyo yao kumtafuta BWANA, Mungu wa Israeli, wakawafuata Walawi huko Yerusalemu kumtolea BWANA dhabihu, Mungu wa baba zao. [17] Wakaimarisha ufalme wa Yuda na kumuunga mkono Rehoboamu mwana wa Solomoni miaka mitatu, wakienenda katika njia za Daudi na Solomoni katika wakati huu. [18] Rehoboamu alimwoa Mahalati ambaye alikuwa binti Yeremothi mwana wa Daudi, mamaye alikuwa Abihaili binti Eliabu mwana wa Yese. [19] Mahalati alimzalia Rehoboamu wana: Yeushi, Shemaria na Zahamu. [20] Kisha akamwoa Maaka binti Absalomu, ambaye alimzalia: Abiya, Atai, Ziza na Shelomithi. [21] Rehoboamu akampenda Maaka binti Absalomu zaidi kuliko wakeze wengine na masuria wake. Kwa jumla alikuwa na wake kumi na wanane na masuria sitini, wana ishirini na wanane na binti sitini. [22] Rehoboamu akamweka Abiya mwana wa Maaka, kuwa mkuu wa wana wa mfalme miongoni mwa ndugu zake ili amfanye mfalme. [23] Akatenda kwa busara, akiwasambaza baadhi ya wanawe katika wilaya zote za Yuda na Benyamini, pamoja na miji yote yenye ngome. Akawapa mahitaji tele na kuwaoza wake wengi.
