[1] Kisha nikatazama juu: pale mbele yangu alikuwepo mtu mwenye kamba ya kupimia mkononi mwake! [2] Nikamuuliza, “Unakwenda wapi?” Akanijibu, “Kupima Yerusalemu, kupata urefu na upana wake.” [3] Kisha malaika aliyekuwa akizungumza nami akaondoka, malaika mwingine akaja kukutana naye [4] na kumwambia: “Kimbia, umwambie yule kijana, ‘Yerusalemu utakuwa mji usio na kuta kwa sababu ya wingi wa watu na mifugo iliyomo. [5] Mimi mwenyewe nitakuwa ukuta wa moto kuuzunguka,’ asema BWANA, ‘nami nitakuwa utukufu wake ndani yake.’ [6] “Njooni! Njooni! Kimbieni mtoke katika nchi ya kaskazini,” asema BWANA, “Kwa kuwa nimewatawanya kwenye pande nne za mbingu,” asema BWANA. [7] “Njoo, ee Sayuni! Kimbia, wewe ukaaye ndani ya Binti Babeli!” [8] Kwa kuwa hivi ndivyo asemavyo BWANA Mwenye Nguvu Zote: “Baada ya yeye kuniheshimu na kunituma mimi dhidi ya mataifa yaliyokuteka nyara, kwa kuwa yeyote awagusaye ninyi, anaigusa mboni ya jicho lake, [9] hakika nitauinua mkono wangu dhidi yao ili watumwa wao wawateke nyara. Ndipo mtakapojua ya kwamba BWANA Mwenye Nguvu Zote amenituma. [10] “Piga kelele na ufurahie, ee Binti Sayuni, kwa maana ninakuja, nami nitaishi miongoni mwenu,” asema BWANA. [11] “Mataifa mengi yataunganishwa na BWANA siku hiyo, nao watakuwa watu wangu. Nitaishi miongoni mwenu nanyi mtajua kwamba BWANA Mwenye Nguvu Zote amenituma kwenu. [12] BWANA atairithi Yuda kama fungu lake katika nchi takatifu na atachagua tena Yerusalemu. [13] Tulieni mbele za BWANA, enyi watu wote, kwa sababu ameinuka kutoka makao yake matakatifu.”