[1] Kwa nini mataifa wanashauriana kufanya mabaya, na kabila za watu kula njama bure? [2] Wafalme wa dunia wanajipanga na watawala wanajikusanya pamoja dhidi ya BWANA na dhidi ya Mpakwa Mafuta wake. [3] Wanasema, “Tuvunje minyororo yao na kuvitupilia mbali vifungo vyao.” [4] Yeye atawalaye mbinguni hucheka, Bwana huwadharau. [5] Kisha huwakemea katika hasira yake na kuwaogopesha katika ghadhabu yake, akisema, [6] “Nimemtawaza Mfalme wangu juu ya Sayuni, mlima wangu mtakatifu.” [7] Nitatangaza amri ya BWANA: Yeye aliniambia, “Wewe ni Mwanangu, leo mimi nimekuzaa. [8] Niombe, nami nitayafanya mataifa kuwa urithi wako, miisho ya dunia kuwa milki yako. [9] Utawatawala kwa fimbo ya chuma na kuwavunjavunja kama chombo cha mfinyanzi.” [10] Kwa hiyo, ninyi wafalme, kuweni na hekima; mwonyeke, enyi watawala wa dunia. [11] Mtumikieni BWANA kwa hofu na mshangilie kwa kutetemeka. [12] Mbusu Mwana, asije akakasirika nawe ukaangamizwa katika njia yako, kwa maana hasira yake inaweza kuwaka ghafula. Heri wote wanaomkimbilia.