[1] Ee Mungu, uniweke salama, kwa maana kwako nimekimbilia. [2] Nilimwambia BWANA, “Wewe ndiwe Bwana wangu; pasipo wewe sina jambo jema.” [3] Kwa habari ya watakatifu walioko duniani, ndio walio wa fahari ambao ninapendezwa nao. [4] Huzuni itaongezeka kwa wale wanaokimbilia miungu mingine. Sitazimimina sadaka zao za damu au kutaja majina yao midomoni mwangu. [5] BWANA umeniwekea fungu langu na kikombe changu; umeyafanya mambo yangu yote yawe salama. [6] Alama za mipaka zimeniangukia mahali pazuri, hakika nimepata urithi mzuri. [7] Nitamsifu BWANA ambaye hunishauri, hata wakati wa usiku moyo wangu hunifundisha. [8] Nimemweka BWANA mbele yangu daima. Kwa sababu yuko mkono wangu wa kuume, sitatikisika. [9] Kwa hiyo moyo wangu unafurahia, na ulimi wangu unashangilia; mwili wangu nao utapumzika salama, [10] kwa maana hutaniacha kaburini, wala hutamwacha Mtakatifu Wako kuona uharibifu. [11] Umenijulisha njia ya uzima; utanijaza na furaha mbele zako, pamoja na furaha za milele katika mkono wako wa kuume.