[1] Ee BWANA, mkumbuke Daudi na taabu zote alizozistahimili. [2] Aliapa kiapo kwa BWANA na akaweka nadhiri kwa Yule Mwenye Nguvu wa Yakobo: [3] “Sitaingia nyumbani mwangu au kwenda kitandani mwangu: [4] sitaruhusu usingizi katika macho yangu, wala kope zangu kusinzia, [5] mpaka nitakapompatia BWANA mahali, makao kwa ajili ya Yule Mwenye Nguvu wa Yakobo.” [6] Tulisikia habari hii huko Efrathi, tulikutana nayo katika mashamba ya Yaara: [7] “Twendeni kwenye makao yake, na tuabudu kwenye kiti cha kuwekea miguu yake; [8] inuka, Ee BWANA, uje mahali pako pa kupumzikia, wewe na Sanduku la nguvu zako. [9] Makuhani wako na wavikwe haki, watakatifu wako na waimbe kwa furaha.” [10] Kwa ajili ya Daudi mtumishi wako, usimkatae mpakwa mafuta wako. [11] BWANA alimwapia Daudi kiapo, kiapo cha uhakika ambacho hatakitangua: “Nitamweka mmoja wa wazao wako mwenyewe katika kiti chako cha enzi, [12] kama wanao watashika Agano langu na sheria ninazowafundisha, ndipo wana wao watarithi kiti chako cha enzi milele na milele.” [13] Kwa maana BWANA ameichagua Sayuni, amepaonea shauku pawe maskani yake: [14] “Hapa ni mahali pangu pa kupumzika milele na milele; hapa ndipo nitakapoketi nikitawala, kwa sababu nimepaonea shauku: [15] Nitambariki kwa kumpa mahitaji tele: nitashibisha maskini wake kwa chakula. [16] Nitawavika makuhani wake wokovu, nao watakatifu wake watadumu wakiimba kwa furaha. [17] “Hapa nitamchipushia Daudi pembe, na kuweka taa kwa ajili ya masiya wangu. [18] Adui zake nitawavika aibu, bali taji kichwani pake itangʼaa sana.”