[1] Msifuni BWANA. Heri mtu yule amchaye BWANA, mtu yule apendezwaye sana na amri zake. [2] Watoto wake watakuwa wenye uwezo katika nchi, kizazi cha watu waadilifu kitabarikiwa. [3] Nyumbani mwake kuna mali na utajiri, haki yake hudumu milele. [4] Hata gizani nuru humzukia mtu mwadilifu, yule mwenye rehema, huruma na haki. [5] Mema yatamjia mtu yule aliye mkarimu na mwenye kukopesha bila riba, anayefanya mambo yake kwa haki. [6] Hakika hatatikisika kamwe, mtu mwenye haki atakumbukwa milele. [7] Hataogopa habari mbaya, moyo wake ni thabiti, ukimtegemea BWANA. [8] Moyo wake ni salama, hatakuwa na hofu, mwishoni ataona ushindi dhidi ya adui zake. [9] Ametawanya vipawa vyake kwa ukarimu akawapa maskini; haki yake hudumu milele; pembe yake itatukuzwa kwa heshima. [10] Mtu mwovu ataona na kuchukizwa, atasaga meno yake na kutoweka, kutamani kwa mtu mwovu kutaishia patupu.