[1] Akiwa ndani ya tumbo la nyangumi, Yona alimwomba BWANA Mungu wake. [2] Akasema: “Katika shida yangu nalimwita BWANA, naye akanijibu. Kutoka kina cha kaburi niliomba msaada, nawe ukasikiliza kilio changu. [3] Ulinitupa kwenye kilindi, ndani kabisa ya moyo wa bahari, mikondo ya maji ilinizunguka, mawimbi yako yote na viwimbi vilipita juu yangu. [4] Nikasema, ‘Nimefukuziwa mbali na uso wako, hata hivyo nitatazama tena kuelekea Hekalu lako takatifu.’ [5] Maji yaliyonimeza yalinitisha, kilindi kilinizunguka; mwani ulijisokota kichwani pangu. [6] Nilizama chini sana mpaka pande za mwisho za milima, makomeo ya hiyo nchi yalinifungia hata milele. Lakini uliuleta uhai wangu kutoka shimoni, Ee BWANA Mungu wangu. [7] “Wakati uhai wangu ulipokuwa unatoka, nilikukumbuka wewe, BWANA, nayo maombi yangu yalikufikia wewe, katika Hekalu lako takatifu. [8] “Wale watu wanaongʼangʼana na sanamu zisizofaa hupoteza neema ile ambayo ingekuwa yao. [9] Lakini mimi, kwa wimbo wa shukrani, nitakutolea dhabihu. Lile nililowekea nadhiri nitalitimiza. Wokovu watoka kwa BWANA.” [10] Basi BWANA akamwamuru yule nyangumi, naye akamtapika Yona katika nchi kavu.