Yoeli 1:1-20 ONEN
[1] Neno la BWANA ambalo lilimjia Yoeli mwana wa Pethueli. [2] Sikilizeni hili, enyi wazee; sikilizeni, ninyi nyote mnaoishi katika nchi. Je, jambo kama hili lilishawahi kutokea katika siku zenu au katika siku za babu zenu? [3] Waelezeni watoto wenu, na watoto wenu wawaambie watoto wao, na watoto wao kwa kizazi kitakachofuata. [4] Kilichosazwa na kundi la tunutu nzige wakubwa wamekula, kilichosazwa na nzige wakubwa parare wamekula, kilichosazwa na parare madumadu wamekula. [5] Amkeni, enyi walevi, mlie! Pigeni yowe enyi wanywaji wote wa mvinyo, pigeni yowe kwa sababu ya mvinyo mpya, kwa kuwa mmenyangʼanywa kutoka midomoni mwenu. [6] Taifa limevamia nchi yangu, lenye nguvu tena lisilo na idadi; lina meno ya simba, magego ya simba jike. [7] Limeharibu mizabibu yangu na kuangamiza mitini yangu. Limebambua magome yake na kuyatupilia mbali, likayaacha matawi yake yakiwa meupe. [8] Omboleza kama bikira aliyevaa nguo ya gunia anayehuzunika kwa ajili ya mume wa ujana wake. [9] Sadaka za nafaka na sadaka za kinywaji zimekatiliwa mbali kutoka nyumba ya BWANA. Makuhani wanaomboleza, wale wanaohudumu mbele za BWANA. [10] Mashamba yameharibiwa, ardhi imekauka; nafaka imeharibiwa, mvinyo mpya umekauka, mafuta yamekoma. [11] Kateni tamaa, enyi wakulima, lieni, enyi mlimao mizabibu; huzunikeni kwa ajili ya ngano na shayiri, kwa sababu mavuno ya shambani yameharibiwa. [12] Mzabibu umekauka na mtini umenyauka; mkomamanga, mtende na mtofaa, miti yote shambani, imekauka. Hakika furaha yote ya mwanadamu imeondoka. [13] Vaeni nguo ya gunia, enyi makuhani, muomboleze; pigeni yowe, enyi mnaohudumu madhabahuni. Njooni, vaeni nguo ya gunia usiku kucha, enyi mnaohudumu mbele za Mungu wangu; kwa kuwa sadaka za nafaka na sadaka za kinywaji zimezuiliwa kufika katika nyumba ya Mungu wenu. [14] Tangazeni saumu takatifu; liiteni kusanyiko takatifu. Iteni wazee na wote waishio katika nchi waende katika nyumba ya BWANA Mungu wenu, wakamlilie BWANA. [15] Ole kwa siku hiyo! Kwa kuwa siku ya BWANA iko karibu; itakuja kama uharibifu kutoka kwa Mwenyezi. [16] Je, chakula hakikukatiliwa mbali mbele ya macho yetu: furaha na shangwe kutoka nyumba ya Mungu wetu? [17] Mbegu zinakauka chini ya mabonge ya udongo. Ghala zimeachwa katika uharibifu, ghala za nafaka zimebomolewa, kwa maana hakuna nafaka. [18] Jinsi gani ngʼombe wanavyolia! Makundi ya mifugo yanahangaika kwa sababu hawana malisho; hata makundi ya kondoo yanateseka. [19] Kwako, Ee BWANA, naita, kwa kuwa moto umeteketeza malisho ya mbugani na miali ya moto imeunguza miti yote shambani. [20] Hata wanyama wa porini wanakuonea shauku; vijito vya maji vimekauka, na moto umeteketeza malisho yote ya mbugani.
