Yeremia 9:1-26 ONEN
[1] Laiti kichwa changu kingekuwa chemchemi ya maji na macho yangu yangekuwa kisima cha machozi! Ningelia usiku na mchana kwa kuuawa kwa watu wangu. [2] Laiti ningekuwa na nyumba ya kukaa wasafiri jangwani, ningewaacha watu wangu na kwenda mbali nao, kwa kuwa wote ni wazinzi, kundi la watu wadanganyifu. [3] “Huweka tayari ndimi zao kama upinde, ili kurusha uongo; wamekuwa na nguvu katika nchi lakini si katika ukweli. Wanatoka dhambi moja hadi nyingine, hawanitambui mimi,” asema BWANA. [4] “Jihadhari na rafiki zako; usiwaamini ndugu zako. Kwa kuwa kila ndugu ni mdanganyifu, na kila rafiki ni msingiziaji. [5] Rafiki humdanganya rafiki, hakuna yeyote asemaye kweli. Wamefundisha ndimi zao kudanganya, wanajichosha wenyewe katika kutenda dhambi. [6] Unakaa katikati ya udanganyifu; katika udanganyifu wao wanakataa kunitambua mimi,” asema BWANA. [7] Kwa hiyo hili ndilo asemalo BWANA Mwenye Nguvu Zote: “Tazama, nitawasafisha na kuwajaribu, kwani ni nini kingine niwezacho kufanya kwa sababu ya dhambi ya watu wangu? [8] Ndimi zao ni mshale wenye sumu, hunena kwa udanganyifu. Kwa kinywa chake kila mmoja huzungumza maneno mazuri na jirani yake, lakini moyoni mwake humtegea mtego. [9] Je, nisiwaadhibu kwa ajili ya jambo hili?” asema BWANA. “Je, nisijilipizie kisasi kwa taifa kama hili?” [10] Nitalia na kuomboleza kwa ajili ya milima na kuomboleza kuhusu malisho ya jangwani. Yamekuwa ukiwa, wala hakuna apitaye humo, milio ya ngʼombe haisikiki. Ndege wa angani wametoroka na wanyama wamekimbia. [11] “Nitaifanya Yerusalemu lundo la magofu, makao ya mbweha; nami nitaifanya miji ya Yuda kuwa ukiwa ili asiwepo atakayeishi humo.” [12] Ni mtu yupi aliye na hekima ya kutosha ayaelewe haya? Ni nani aliyefundishwa na BWANA awezaye kuyaeleza haya? Kwa nini nchi imeharibiwa na kufanywa ukiwa kama jangwa ambapo hakuna awezaye kupita? [13] BWANA akasema, “Ni kwa sababu wameiacha sheria yangu, niliyoiweka mbele yao: hawajaniheshimu mimi wala kufuata sheria yangu. [14] Badala yake wamefuata ukaidi wa mioyo yao, wamefuata Mabaali, kama vile baba zao walivyowafundisha.” [15] Kwa hiyo, hivi ndivyo asemavyo BWANA Mwenye Nguvu Zote, Mungu wa Israeli: “Tazama, nitawafanya watu hawa wale chakula kichungu na kunywa maji yenye sumu. [16] Nitawatawanya katika mataifa ambayo wao wala baba zao hawakuwajua, nikiwafuata kwa upanga mpaka niwe nimewaangamiza kabisa.” [17] Hivi ndivyo asemavyo BWANA Mwenye Nguvu Zote: “Fikiri sasa! Waite wanawake waombolezao waje, waite wale walio na ustadi kuliko wote. [18] Nao waje upesi na kutuombolezea, mpaka macho yetu yafurike machozi na vijito vya maji vitoke kwenye kope zetu. [19] Sauti ya kuomboleza imesikika kutoka Sayuni: ‘Tazama jinsi tulivyoangamizwa! Tazama jinsi aibu yetu ilivyo kubwa! Ni lazima tuihame nchi yetu kwa sababu nyumba zetu zimekuwa magofu.’ ” [20] Basi, enyi wanawake, sikieni neno la BWANA; fungueni masikio yenu msikie maneno ya kinywa chake. Wafundisheni binti zenu kuomboleza; fundishaneni kila mmoja na mwenzake maombolezo. [21] Mauti imeingia ndani kupitia madirishani, imeingia kwenye majumba yetu ya fahari; imewakatilia mbali watoto katika barabara na vijana waume kutoka viwanja vya miji. [22] Sema, “Hili ndilo asemalo BWANA: “ ‘Maiti za wanaume zitalala kama mavi katika mashamba, kama malundo ya nafaka nyuma ya mvunaji, wala hakuna anayekusanya.’ ” [23] Hili ndilo asemalo BWANA: “Mwenye hekima asijisifu katika hekima yake, au mwenye nguvu ajisifu katika nguvu zake, wala tajiri ajisifu katika utajiri wake, [24] lakini yeye ajisifuye, na ajisifu kwa sababu hili: kwamba ananifahamu na kunijua mimi, kwamba mimi ndimi BWANA, nitendaye wema, hukumu na haki duniani, kwa kuwa napendezwa na haya,” asema BWANA. [25] “Siku zinakuja, nitakapowaadhibu wale wote ambao wametahiriwa kimwili tu, asema BWANA, [26] yaani Misri, Yuda, Edomu, Amoni, Moabu na wote wanaoishi jangwani sehemu za mbali. Kwa maana mataifa haya yote hayakutahiriwa mioyo yao, nayo nyumba yote ya Israeli haikutahiriwa.”
