Yeremia 51:1-64 ONEN
[1] Hili ndilo asemalo BWANA: “Tazama nitaamsha roho ya mwangamizi dhidi ya Babeli na watu wakaao Leb-Kamai. [2] Nitawatuma wageni Babeli kumpepeta na kuiharibu nchi yake; watampinga kila upande katika siku ya maafa yake. [3] Usimwache mpiga upinde afunge kamba upinde wake, wala usimwache avae silaha zake. Usiwaonee huruma vijana wake; angamiza jeshi lake kabisa. [4] Wataanguka waliouawa katika Babeli, wakiwa na majeraha ya kutisha barabarani zake. [5] Kwa maana Israeli na Yuda hawajaachwa na Mungu wao, BWANA Mwenye Nguvu Zote, ingawa nchi yao imejaa uovu mbele zake yeye Aliye Mtakatifu wa Israeli. [6] “Kimbieni kutoka Babeli! Okoeni maisha yenu! Msiangamizwe kwa sababu ya dhambi zake. Ni wakati wa kisasi cha BWANA, atamlipa kile anachostahili. [7] Babeli alikuwa kikombe cha dhahabu katika mkono wa BWANA; aliufanya ulimwengu wote ulewe. Mataifa walikunywa mvinyo wake; kwa hiyo sasa wameingiwa na wazimu. [8] Babeli ataanguka ghafula na kuvunjika. Mwombolezeni! Tafuteni zeri ya kutuliza maumivu yake, labda anaweza kupona. [9] “ ‘Tungemponya Babeli, lakini hawezi kuponyeka; tumwacheni, na kila mmoja wetu aende nchi yake mwenyewe, kwa kuwa hukumu yake inafika angani, inapanda juu hadi mawinguni.’ [10] “ ‘BWANA amethibitisha haki yetu; njooni, tutangaze katika Sayuni kitu ambacho BWANA Mungu wetu amefanya.’ [11] “Noeni mishale, chukueni ngao! BWANA amewaamsha wafalme wa Wamedi, kwa sababu nia yake ni kuangamiza Babeli. BWANA atalipiza kisasi, kisasi kwa ajili ya Hekalu lake. [12] Twekeni bendera juu ya kuta za Babeli! Imarisheni ulinzi, wekeni walinzi, andaeni waviziao! BWANA atatimiza kusudi lake, amri yake juu ya watu wa Babeli. [13] Wewe uishiye kando ya maji mengi na uliye na wingi wa hazina, mwisho wako umekuja, wakati wako wa kukatiliwa mbali. [14] BWANA Mwenye Nguvu Zote ameapa kwa nafsi yake mwenyewe: ‘Hakika nitakujaza na watu, kama kundi la nzige, nao watapiga kelele za ushindi juu yako.’ [15] “Aliiumba dunia kwa uweza wake; akaweka misingi ya ulimwengu kwa hekima yake na akazitandaza mbingu kwa ufahamu wake. [16] Atoapo sauti yake, maji yaliyo katika mbingu hunguruma, huyafanya mawingu yainuke kutoka miisho ya dunia. Hupeleka umeme wa radi pamoja na mvua, naye huuleta upepo kutoka ghala zake. [17] “Kila mtu ni mjinga na hana maarifa; kila sonara ameaibishwa na sanamu zake. Vinyago vyake ni vya udanganyifu, havina pumzi ndani yavyo. [18] Havifai kitu, ni vitu vya kufanyia mzaha, hukumu yavyo itakapowadia, vitaangamia. [19] Yeye Aliye Fungu la Yakobo sivyo alivyo, kwani ndiye Muumba wa vitu vyote, pamoja na kabila la urithi wake: BWANA Mwenye Nguvu Zote ndilo jina lake. [20] “Wewe ndiwe rungu langu la vita, silaha yangu ya vita: kwa wewe navunjavunja mataifa, kwa wewe naangamiza falme, [21] kwa wewe navunjavunja farasi na mpanda farasi, kwa wewe navunjavunja gari la vita na mwendeshaji wake, [22] kwa wewe napondaponda mwanaume na mwanamke, kwa wewe napondaponda mzee na kijana, kwa wewe napondaponda kijana wa kiume na mwanamwali, [23] kwa wewe nampondaponda mchungaji na kundi, kwa wewe nampondaponda mkulima na maksai, kwa wewe nawapondaponda watawala na maafisa. [24] “Mbele ya macho yako nitamlipiza Babeli na wote waishio Ukaldayo kwa ajili ya makosa yote waliyofanya katika Sayuni,” asema BWANA. [25] “Mimi niko kinyume nawe, ee mlima unaoharibu, wewe uangamizaye dunia yote,” asema BWANA. “Nitanyoosha mkono wangu dhidi yako, nikuvingirishe kutoka kwenye kilele cha mwamba, na kukufanya mlima ulioteketezwa kwa moto. [26] Hakuna jiwe litakalochukuliwa kutoka kwako kwa ajili ya kufanywa jiwe la pembeni, wala jiwe lolote kwa ajili ya msingi, kwa maana utakuwa ukiwa milele,” asema BWANA. [27] “Twekeni bendera katika nchi! Pigeni tarumbeta katikati ya mataifa! Andaeni mataifa kwa ajili ya vita dhidi yake, iteni falme hizi dhidi yake: Ararati, Mini na Ashkenazi. Wekeni jemadari dhidi yake, pelekeni farasi wengi kama kundi la nzige. [28] Andaeni mataifa kwa ajili ya vita dhidi yake, wafalme wa Wamedi, watawala wao na maafisa wao wote, pamoja na nchi zote wanazotawala. [29] Nchi inatetemeka na kugaagaa, kwa kuwa makusudi ya BWANA dhidi ya Babeli yanasimama: yaani, kuangamiza nchi ya Babeli ili pasiwe na yeyote atakayeishi humo. [30] Mashujaa wa Babeli wameacha kupigana, wamebaki katika ngome zao. Nguvu zao zimekwisha, wamekuwa kama wanawake. Makazi yake yameteketezwa kwa moto, makomeo ya malango yake yamevunjika. [31] Tarishi mmoja humfuata mwingine, na mjumbe humfuata mjumbe, kumtangazia mfalme wa Babeli kwamba mji wake wote umetekwa, [32] Vivuko vya mito vimekamatwa, mabwawa yenye mafunjo yametiwa moto, nao askari wameingiwa na hofu kuu.” [33] Hili ndilo BWANA Mwenye Nguvu Zote, Mungu wa Israeli, asemalo: “Binti Babeli ni kama sakafu ya kupuria wakati inapokanyagwa; wakati wa kumvuna utakuja upesi.” [34] “Nebukadneza mfalme wa Babeli ametula, ametufanya tuchangayikiwe, ametufanya tuwe gudulia tupu. Kama nyoka ametumeza na kujaza tumbo lake kwa vyakula vyetu vizuri, kisha akatutapika. [35] Jeuri iliyofanyiwa miili yetu na iwe juu ya Babeli,” ndivyo wasemavyo wakaao Sayuni. “Damu yetu na iwe juu ya wale waishio Babeli,” asema Yerusalemu. [36] Kwa hiyo, hili ndilo BWANA asemalo: “Tazama, nitatetea shauri lako na kulipiza kisasi kwa ajili yako; nitaikausha bahari yake na kuzikausha chemchemi zake. [37] Babeli utakuwa lundo la magofu na makao ya mbweha, kitu cha kutisha na kudharauliwa, mahali asipoishi mtu. [38] Watu wake wote wananguruma kama simba wadogo, wanakoroma kama wana simba. [39] Lakini wakati wakiwa wameamshwa, nitawaandalia karamu na kuwafanya walewe, ili wapige kelele kwa kicheko, kisha walale milele na wasiamke,” asema BWANA. [40] “Nitawateremsha kama wana-kondoo waendao machinjoni, kama kondoo dume na mbuzi. [41] “Tazama jinsi Sheshaki atakamatwa, majivuno ya dunia yote yatakavyonyakuliwa. Babeli atakuwa mwenye hofu kiasi gani kati ya mataifa! [42] Bahari itainuka juu ya Babeli; mawimbi yake yenye kunguruma yatamfunika. [43] Miji yake itakuwa ukiwa, kame na jangwa, nchi ambayo hakuna yeyote anayeishi ndani yake, ambayo hakuna mtu anayepita humo. [44] Nitamwadhibu Beli katika Babeli, na kumfanya atapike kile alichokimeza. Mataifa hayatamiminika tena kwake. Nao ukuta wa Babeli utaanguka. [45] “Tokeni ndani yake, enyi watu wangu! Okoeni maisha yenu! Ikimbieni hasira kali ya BWANA. [46] Msikate tamaa wala msiogope tetesi zitakaposikika katika nchi; tetesi moja inasikika mwaka huu, nyingine mwaka unaofuata; tetesi juu ya jeuri katika nchi, na ya mtawala dhidi ya mtawala. [47] Kwa kuwa hakika wakati utawadia nitakapoziadhibu sanamu za Babeli; nchi yake yote itatiwa aibu, na watu wake wote waliouawa wataangukia ndani yake. [48] Ndipo mbingu na dunia na vyote vilivyomo ndani yake vitapiga kelele za shangwe juu ya Babeli, kwa kuwa kutoka kaskazini waharabu watamshambulia,” asema BWANA. [49] “Babeli ni lazima aanguke kwa sababu ya kuwaua Waisraeli, kama vile waliouawa duniani kote walivyoanguka kwa sababu ya Babeli. [50] Wewe uliyepona upanga, ondoka wala usikawie! Mkumbuke BWANA ukiwa katika nchi ya mbali, na utafakari juu ya Yerusalemu.” [51] “Tumetahayari, kwa maana tumetukanwa na aibu imefunika nyuso zetu, kwa sababu wageni wameingia mahali patakatifu pa nyumba ya BWANA.” [52] “Lakini siku zinakuja,” asema BWANA, “nitakapoadhibu sanamu zake, na katika nchi yake yote waliojeruhiwa watalia kwa maumivu makali. [53] Hata kama Babeli ikifika angani na kuziimarisha ngome zake ndefu, nitatuma waharabu dhidi yake,” asema BWANA. [54] “Sauti ya kilio inasikika kutoka Babeli, sauti ya uharibifu mkuu kutoka nchi ya Wakaldayo. [55] BWANA ataiangamiza Babeli, atanyamazisha makelele ya kishindo chake. Mawimbi ya adui yatanguruma kama maji makuu, ngurumo ya sauti zao itavuma. [56] Mharabu atakuja dhidi ya Babeli, mashujaa wake watakamatwa, nazo pinde zao zitavunjwa. Kwa kuwa BWANA ni Mungu wa kisasi, yeye atalipiza kikamilifu. [57] Nitawafanya maafisa wake na wenye busara walewe, watawala wao, maafisa, pamoja na wapiganaji wao; watalala milele na hawataamka,” asema Mfalme, ambaye jina lake ni BWANA Mwenye Nguvu Zote. [58] Hili ndilo BWANA Mwenye Nguvu Zote asemalo: “Ukuta mnene wa Babeli utasawazishwa, na malango yaliyoinuka yatateketezwa kwa moto; mataifa yanajichosha bure, taabu ya mataifa ni nishati tu ya miali ya moto.” [59] Huu ndio ujumbe Yeremia aliompa afisa Seraya mwana wa Neria mwana wa Maaseya, alipokwenda Babeli pamoja na Sedekia mfalme wa Yuda, katika mwaka wa nne wa utawala wake. [60] Yeremia alikuwa ameandika ndani ya kitabu kuhusu maafa yote yatakayoipata Babeli, yaani yote yaliyokuwa yameandikwa kuhusu Babeli. [61] Yeremia akamwambia Seraya, “Utakapofika Babeli, hakikisha kwamba umesoma maneno haya yote kwa sauti kubwa. [62] Kisha sema, ‘Ee BWANA, umesema utaangamiza mahali hapa ili mtu wala mnyama asiishi ndani yake, napo patakuwa ukiwa milele.’ [63] Utakapomaliza kusoma hiki kitabu, kifungie jiwe kisha ukitupe ndani ya Mto Frati. [64] Kisha sema, ‘Hivi ndivyo Babeli utakavyozama na usiinuke tena, kwa sababu ya maafa nitakayoleta juu yake. Nao watu wake wataanguka.’ ” Maneno ya Yeremia yanaishia hapa.
