[1] Hili ndilo neno la BWANA lililomjia nabii Yeremia kuhusu Wafilisti, kabla Farao hajaishambulia Gaza: [2] Hili ndilo asemalo BWANA: “Tazama jinsi maji yanavyoinuka huko kaskazini, yatakuwa mafuriko yenye nguvu sana. Yataifurikia nchi na vitu vyote vilivyomo ndani yake, miji na wale waishio ndani yake. Watu watapiga kelele; wote waishio katika nchi wataomboleza [3] kwa sauti ya kwato za farasi waendao mbio, kwa sauti ya magari ya adui na mngurumo wa magurudumu yake. Baba hawatageuka kuwasaidia watoto wao, mikono yao italegea. [4] Kwa maana siku imewadia kuwaangamiza Wafilisti wote na kuwakatilia mbali walionusurika wote ambao wangeweza kusaidia Tiro na Sidoni. BWANA anakaribia kuwaangamiza Wafilisti, mabaki toka pwani za Kaftori. [5] Gaza atanyoa kichwa chake katika kuomboleza, Ashkeloni atanyamazishwa. Enyi mabaki kwenye tambarare, mtajikatakata wenyewe mpaka lini? [6] “Mnalia, ‘Aa, upanga wa BWANA, utaendelea mpaka lini ndipo upumzike? Rudi ndani ya ala yako; acha na utulie.’ [7] Lakini upanga utatuliaje wakati BWANA ameuamuru, wakati ameuagiza kuishambulia Ashkeloni pamoja na pwani yake?”