Yeremia 18:1-23 ONEN
[1] Hili ndilo neno lililomjia Yeremia kutoka kwa BWANA: [2] “Shuka uende mpaka nyumba ya mfinyanzi, nami huko nitakupa ujumbe wangu.” [3] Kwa hiyo nikashuka mpaka kwenye nyumba ya mfinyanzi, nikamkuta akifinyanga kwa gurudumu lake. [4] Lakini chombo alichokuwa akikifinyanga kutokana na udongo kilivunjika mikononi mwake, hivyo mfinyanzi akakifanya kuwa chombo kingine, umbo jingine kama vile ilivyoonekana vyema kwake yeye. [5] Kisha neno la BWANA likanijia kusema: [6] “Ee nyumba ya Israeli, je, siwezi kuwafanyia kama huyu mfinyanzi afanyavyo?” asema BWANA. “Kama vile udongo ulivyo katika mikono ya mfinyanzi, ndivyo mlivyo katika mkono wangu, ee nyumba ya Israeli. [7] Ikiwa wakati wowote nikitangaza kuwa taifa au ufalme utangʼolewa, utaangushwa na kuangamizwa, [8] ikiwa lile taifa nililolionya litatubia uovu wake, ndipo nitakapokuwa na huruma, wala sitawapiga kwa maafa niliyokuwa nimewakusudia. [9] Ikiwa wakati mwingine nitatangaza kuwa taifa ama utawala ujengwe na kuwekwa wakfu, [10] ikiwa utafanya maovu mbele zangu na hukunitii, ndipo nitakapoghairi makusudio yangu mema niliyokuwa nimeyakusudia. [11] “Basi kwa hiyo waambie watu wa Yuda na wale waishio Yerusalemu, ‘Hili ndilo asemalo BWANA: Tazama! Ninaandaa maafa kwa ajili yenu, nami ninabuni mabaya dhidi yenu. Kwa hiyo geukeni kutoka njia zenu mbaya, kila mmoja wenu, tengenezeni njia zenu na matendo yenu.’ [12] Lakini wao watajibu, ‘Hakuna faida. Tutaendelea na mipango yetu wenyewe, kila mmoja wetu atafuata ukaidi wa moyo wake mbaya.’ ” [13] Kwa hiyo hili ndilo asemalo BWANA: “Ulizia miongoni mwa mataifa: Ni nani alishasikia jambo kama hili? Jambo la kutisha sana limefanywa na Bikira Israeli. [14] Je, barafu ya Lebanoni iliwahi kutoweka kwenye miteremko yake ya mawe wakati wowote? Je, maji yake baridi yatokayo katika vyanzo vilivyo mbali yaliwahi kukoma kutiririka wakati wowote? [15] Lakini watu wangu wamenisahau mimi, wanafukizia uvumba sanamu zisizofaa kitu, zilizowafanya wajikwae katika njia zao na katika mapito ya zamani. Zimewafanya wapite kwenye vichochoro na kwenye barabara ambazo hazikujengwa. [16] Nchi yao itaharibiwa, itakuwa kitu cha kudharauliwa daima; wote wapitao karibu nayo watashangaa na kutikisa vichwa vyao. [17] Kama upepo utokao mashariki, nitawatawanya mbele ya adui zao; nitawapa kisogo wala sio uso, katika siku ya maafa yao.” [18] Wakasema, “Njooni, tutunge hila dhidi ya Yeremia; kwa kuwa kufundisha sheria kwa kuhani hakutapotea, wala shauri litokalo kwa mwenye hekima, wala neno la manabii. Hivyo njooni, tumshambulie kwa ndimi zetu na tusijali chochote asemacho.” [19] Nisikilize, Ee BWANA, sikia wanayosema washtaki wangu! [20] Je, mema yalipwe kwa mabaya? Lakini wao wamenichimbia shimo. Kumbuka kwamba nilisimama mbele yako na kunena mema kwa ajili yao, ili wewe ugeuze hasira yako kali mbali nao. [21] Kwa hiyo uwaache watoto wao waone njaa; uwaache wauawe kwa makali ya upanga. Wake zao wasiwe na watoto, na wawe wajane; waume wao wauawe, nao vijana wao waume wachinjwe kwa upanga vitani. [22] Kilio na kisikike kutoka kwenye nyumba zao ghafula uwaletapo adui dhidi yao, kwa kuwa wamechimba shimo ili kunikamata na wameitegea miguu yangu mitego. [23] Lakini unajua, Ee BWANA, hila zao zote za kuniua. Usiyasamehe makosa yao wala usifute dhambi zao mbele za macho yako. Wao na waangamizwe mbele zako; uwashughulikie wakati wa hasira yako.
