[1] Mimi ni ua la Sharoni, yungiyungi ya bondeni. [2] Kama yungiyungi katikati ya miiba ndivyo alivyo mpenzi wangu katikati ya wanawali. [3] Kama mti wa mtofaa miongoni mwa miti ya msituni ndivyo alivyo mpenzi wangu miongoni mwa wanaume vijana. Ninafurahia kuketi kivulini mwa mwanaume huyu, na tunda lake ni tamu kwangu. [4] Amenichukua mpaka kwenye ukumbi wa karamu, na bendera ya huyu mwanaume juu yangu ni upendo. [5] Nitie nguvu kwa zabibu kavu, niburudishe kwa matofaa, kwa maana ninazimia kwa mapenzi. [6] Mkono wake wa kushoto uko chini ya kichwa changu, na mkono wake wa kuume unanikumbatia. [7] Binti za Yerusalemu, ninawaagiza kwa paa na kwa ayala wa shambani: Msichochee wala kuamsha mapenzi hata yatakapotaka yenyewe. [8] Sikiliza! Mpenzi wangu! Tazama! Huyu hapa anakuja, akirukaruka juu milimani akizunguka juu ya vilima. [9] Mpenzi wangu ni kama paa au ayala kijana. Tazama! Anasimama nyuma ya ukuta wetu, akitazama kupitia madirishani, akichungulia kimiani. [10] Mpenzi wangu alizungumza na kuniambia, “Inuka, mpenzi wangu, mrembo wangu, tufuatane. [11] Tazama! Wakati wa masika umepita, mvua imekwisha na ikapita. [12] Maua yanatokea juu ya nchi; majira ya kuimba yamewadia, sauti za njiwa zinasikika katika nchi yetu. [13] Mtini unatunga matunda yake ya mwanzoni, zabibu zinazochanua zaeneza harufu nzuri. Inuka, njoo mpenzi wangu. Mrembo wangu, tufuatane.” [14] Hua wangu penye nyufa za majabali, mafichoni pembezoni mwa mlima, nionyeshe uso wako, na niisikie sauti yako, kwa maana sauti yako ni tamu, na uso wako unapendeza. [15] Tukamatie mbweha, mbweha wale wadogo wanaoharibu mashamba ya mizabibu, mashamba yetu ya mizabibu yaliyochanua. [16] Mpenzi wangu ni wangu, nami ni wake, yeye hujilisha katikati ya yungiyungi. [17] Mpaka jua linapochomoza, na vivuli vikimbie, rudi, mpenzi wangu, na uwe kama paa, au kama ayala kijana juu ya vilima vya Betheri.