Warumi 16:1-27 ONEN
[1] Napenda kumtambulisha kwenu dada yetu Foibe, mtumishi katika kanisa la Kenkrea. [2] Naomba mpokeeni katika Bwana ipasavyo watakatifu na kumpa msaada wowote atakaohitaji kutoka kwenu, kwa maana yeye amekuwa msaada kwa watu wengi, mimi nikiwa miongoni mwao. [3] Wasalimuni Prisila na Akila, watumishi wenzangu katika Kristo Yesu. [4] Wao walihatarisha maisha yao kwa ajili yangu; wala si mimi tu ninayewashukuru bali pia makanisa yote ya watu wa Mataifa. [5] Lisalimuni pia kanisa linalokutana nyumbani mwao. Msalimuni rafiki yangu mpendwa Epaineto, aliyekuwa mtu wa kwanza kumwamini Kristo huko Asia. [6] Msalimuni Maria, aliyefanya kazi kwa bidii kwa ajili yenu. [7] Wasalimuni Androniko na Yunia, jamaa zangu ambao wamekuwa gerezani pamoja nami. Wao ni maarufu miongoni mwa mitume, nao walikuwa katika Kristo kabla yangu. [8] Msalimuni Ampliato, yeye nimpendaye katika Bwana. [9] Msalimuni Urbano, mtendakazi mwenzetu katika Kristo, pamoja na rafiki yangu mpendwa Stakisi. [10] Msalimuni Apele aliyejaribiwa na akaithibitisha imani yake katika Kristo. Wasalimuni wote walio nyumbani mwa Aristobulo. [11] Msalimuni ndugu yangu Herodioni. Wasalimuni wote walio nyumbani mwa Narkisi walio katika Bwana. [12] Wasalimuni Trifaina na Trifosa, wale wanawake wanaofanya kazi kwa bidii katika Bwana. Msalimuni rafiki yangu mpendwa Persisi, mwanamke mwingine aliyefanya kazi kwa bidii katika Bwana. [13] Msalimuni Rufo, mteule katika Bwana, pamoja na mama yake, ambaye amekuwa mama kwangu pia. [14] Wasalimuni Asinkrito, Flegoni, Herme, Patroba, Herma na ndugu wote walio pamoja nao. [15] Wasalimuni Filologo, Yulia, Nerea na dada yake, na Olimpa na watakatifu wote walio pamoja nao. [16] Salimianeni ninyi kwa ninyi kwa busu takatifu. Makanisa yote ya Kristo yanawasalimu. [17] Ndugu zangu, nawasihi mjihadhari na kujiepusha na wale watu waletao matengano na kuweka vikwazo mbele yenu dhidi ya mafundisho mliyojifunza. [18] Kwa maana watu kama hao hawamtumikii Bwana Kristo, bali wanatumikia tamaa zao wenyewe. Kwa kutumia maneno laini na ya kubembeleza, hupotosha mioyo ya watu wajinga. [19] Kila mtu amesikia juu ya utii wenu, nami nimejawa na furaha tele kwa ajili yenu. Lakini nataka mwe na hekima katika mambo mema na bila hatia katika mambo maovu. [20] Mungu wa amani atamponda Shetani chini ya miguu yenu upesi. Neema ya Bwana wetu Yesu iwe nanyi. Amen. [21] Timotheo, mtendakazi mwenzangu anawasalimu. Vivyo hivyo Lukio, Yasoni, na Sosipatro, ndugu zangu. [22] Mimi, Tertio, niliye mwandishi wa waraka huu, nawasalimu katika Bwana. [23] Gayo, ambaye ni mwenyeji wangu na wa kanisa lote, anawasalimu. Erasto, mweka hazina wa mji huu, pamoja na Kwarto ndugu yetu pia wanawasalimu. [ [24] Neema ya Bwana wetu Yesu Kristo iwe pamoja nanyi nyote. Amen.] [25] Sasa atukuzwe yeye awezaye kuwafanya ninyi imara kwa Injili yangu na kuhubiriwa kwa Yesu Kristo, kutokana na kufunuliwa siri zilizofichika tangu zamani za kale. [26] Lakini sasa siri hiyo imefunuliwa na kujulikana kupitia maandiko ya kinabii kutokana na amri ya Mungu wa milele, ili mataifa yote yaweze kumwamini na kumtii [27] Mungu aliye pekee, mwenye hekima, ambaye kwa njia ya Yesu Kristo utukufu ni wake milele na milele! Amen.
