[1] “ ‘Kama sadaka ya mtu ni sadaka ya amani, naye akatoa ngʼombe kutoka kundi, akiwa dume au jike, atamleta mnyama asiye na dosari mbele za BWANA. [2] Ataweka mkono wake juu ya kichwa cha sadaka yake na kumchinja penye ingilio la Hema la Kukutania. Ndipo makuhani wana wa Aroni watanyunyiza damu yake pande zote za madhabahu. [3] Kutoka kwenye hiyo sadaka ya amani ataleta sadaka iliyotolewa kwa BWANA kwa moto: mafuta yote ya mnyama yafunikayo sehemu za ndani, ama yanayoungana na hizo sehemu za ndani, [4] figo zote pamoja na mafuta yote yanayozizunguka karibu na kiuno na yale yanayofunika ini, ambayo atayaondoa pamoja na figo. [5] Kisha wana wa Aroni wataiteketeza juu ya madhabahu, juu ya ile sadaka ya kuteketezwa iliyoko juu ya kuni zinazowaka, kama sadaka ya kuteketezwa kwa moto, harufu nzuri ya kumpendeza BWANA. [6] “ ‘Kama akitoa kondoo au mbuzi kutoka kundi kama sadaka ya amani kwa BWANA, atamtoa dume au jike asiye na dosari. [7] Kama akimtoa mwana-kondoo, atamleta mbele za BWANA. [8] Ataweka mkono wake juu ya kichwa cha sadaka yake, naye atamchinja mbele ya Hema la Kukutania. Kisha wana wa Aroni watanyunyiza damu yake kwenye madhabahu pande zote. [9] Kutoka kwenye hiyo sadaka ya amani ataleta dhabihu iliyotolewa kwa BWANA kwa moto: mafuta yake, mafuta yote ya mkia uliokatwa karibu na uti wa mgongo, mafuta yote yanayofunika sehemu za ndani au yale yanayounganika nazo, [10] figo mbili pamoja na mafuta yanayozizunguka yaliyo karibu na kiuno na yale yanayofunika ini, ambayo atayatoa pamoja na figo. [11] Kuhani ataviteketeza juu ya madhabahu kama chakula, sadaka iliyotolewa kwa BWANA kwa moto. [12] “ ‘Kama sadaka yake ni mbuzi, ataileta mbele za BWANA. [13] Ataweka mkono wake juu ya kichwa chake na kumchinja mbele ya Hema la Kukutania. Kisha wana wa Aroni watanyunyiza damu yake kwenye madhabahu pande zote. [14] Kutokana na ile sadaka anayotoa, atatoa sadaka hii kwa BWANA kwa moto: mafuta yote yanayofunika sehemu za ndani na yale yanayoungana nazo, [15] figo zote mbili pamoja na mafuta yaliyo juu yake karibu na kiuno na yanayofunika ini, ambayo atayaondoa pamoja na figo. [16] Kuhani ataviteketeza juu ya madhabahu kama chakula, sadaka iliyotolewa kwa moto, harufu nzuri. Mafuta yote ya mnyama ni ya BWANA. [17] “ ‘Hii ni kanuni ya kudumu kwa vizazi vijavyo, popote muishipo: Msile mafuta yoyote ya mnyama wala damu.’ ”