Wagalatia 5:1-26 ONEN
[1] Kristo alitupa uhuru, akataka tubaki huru. Hivyo simameni imara wala msikubali tena kulemewa na kongwa la utumwa. [2] Sikilizeni! Mimi, Paulo, nawaambieni kwamba kama mkikubali kutahiriwa, basi Kristo hatawafaidia chochote. [3] Namshuhudia tena kila mtu anayekubali kutahiriwa kwamba inampasa kushika sheria yote. [4] Ninyi mnaotafuta kuhesabiwa haki kwa njia ya sheria mmetengwa na Kristo, mko mbali na neema ya Mungu. [5] Kwa maana, kwa njia ya Roho kwa imani, tunangojea kwa shauku tumaini la haki. [6] Kwa maana ndani ya Kristo Yesu, kutahiriwa au kutokutahiriwa hakuleti tofauti, bali lililo muhimu ni imani itendayo kazi kwa njia ya upendo. [7] Mlikuwa mkipiga mbio vizuri. Ni nani aliyewazuia msiitii kweli? [8] Ushawishi wa namna hiyo haukutokana na yule anayewaita. [9] “Chachu kidogo huchachua donge zima.” [10] Nina hakika katika Bwana kwamba hamtakuwa na msimamo mwingine. Mtu anayewachanganya anastahili adhabu, hata awe nani. [11] Lakini ndugu zangu, kama mimi bado ninahubiri kuhusu kutahiriwa, kwa nini bado ninateswa? Katika hiyo hali basi, kwazo la msalaba limeondolewa. [12] Laiti hao wanaowavuruga wangejihasi wao wenyewe! [13] Ndugu zangu, ninyi mliitwa ili mwe huru, hivyo msitumie uhuru wenu kama fursa ya kufuata tamaa za mwili, bali tumikianeni ninyi kwa ninyi kwa upendo. [14] Kwa maana sheria yote hukamilika katika amri moja: “Mpende jirani yako kama nafsi yako.” [15] Kama mkiumana na kutafunana, angalieni, msije mkaangamizana. [16] Kwa hiyo nasema, enendeni kwa Roho, wala hamtazitimiza kamwe tamaa za mwili. [17] Kwa maana mwili hutamani yale yaliyo kinyume na Roho, naye Roho hutamani yale yaliyo kinyume na mwili. Roho na mwili hupingana na kwa sababu hiyo hamwezi kufanya mnayotaka. [18] Lakini kama mkiongozwa na Roho, hamko chini ya sheria. [19] Basi matendo ya mwili ni dhahiri nayo ni haya: Uasherati, uchafu, ufisadi, [20] kuabudu sanamu, uchawi, uadui, ugomvi, wivu, hasira, fitina, faraka, uzushi, [21] husuda, ulevi, ulafi na mambo mengine yanayofanana na hayo. Nawaonya, kama nilivyokwisha kuwaonya kabla, kwamba watu watendao mambo kama hayo, hawataurithi Ufalme wa Mungu. [22] Lakini tunda la Roho ni upendo, furaha, amani, uvumilivu, utu wema, fadhili, uaminifu, [23] upole na kiasi. Katika mambo kama haya hakuna sheria. [24] Wote walio wa Kristo Yesu wameusulubisha mwili na shauku zake pamoja na tamaa zake. [25] Kwa kuwa tunaishi kwa Roho, basi, tuenende kwa Roho. [26] Tusijisifu bure, tukichokozana na kuoneana wivu.
