[1] Kwa hiyo ndugu watakatifu, mnaoshiriki mwito wa mbinguni, mtafakarini Yesu, mtume na Kuhani Mkuu wa ukiri wetu. [2] Alikuwa mwaminifu kwa yeye aliyemweka, kama vile Mose alivyokuwa mwaminifu katika nyumba yote ya Mungu. [3] Yesu ameonekana anastahili heshima kubwa kuliko Mose, kama vile mjenzi wa nyumba alivyo wa heshima kubwa kuliko nyumba yenyewe. [4] Kwa kuwa kila nyumba hujengwa na mtu fulani, lakini Mungu ni mjenzi wa kila kitu. [5] Basi Mose kama mtumishi alikuwa mwaminifu katika nyumba yote ya Mungu, akishuhudia kwa yale ambayo yangetamkwa baadaye. [6] Lakini Kristo ni mwaminifu kama Mwana katika nyumba ya Mungu. Sisi ndio nyumba yake, kama tutashikilia sana ujasiri wetu na tumaini tunalojivunia. [7] Kwa hiyo, kama Roho Mtakatifu asemavyo: “Leo, kama mkiisikia sauti yake, [8] msiifanye mioyo yenu migumu, kama mlivyofanya katika uasi, wakati ule wa kujaribiwa jangwani, [9] ambapo baba zenu walinijaribu na kunipima ingawa kwa miaka arobaini walikuwa wameyaona matendo yangu. [10] Hiyo ndiyo sababu nilikasirikia kizazi kile, nami nikasema, ‘Siku zote mioyo yao imepotoka, nao hawajazijua njia zangu.’ [11] Hivyo nikatangaza kwa kiapo katika hasira yangu, ‘Kamwe hawataingia rahani mwangu.’ ” [12] Ndugu zangu, angalieni, asiwepo miongoni mwenu mtu mwenye moyo mwovu usioamini, unaojitenga na Mungu aliye hai. [13] Lakini mtiane moyo mtu na mwenzake kila siku, maadamu iitwapo Leo, ili asiwepo hata mmoja wenu mwenye kufanywa mgumu kwa udanganyifu wa dhambi. [14] Kwa kuwa tumekuwa washiriki wa Kristo, kama tukishikamana tu kwa uthabiti na tumaini letu la kwanza hadi mwisho. [15] Kama ilivyonenwa: “Leo, kama mkiisikia sauti yake, msiifanye mioyo yenu migumu kama mlivyofanya wakati wa kuasi.” [16] Basi ni nani waliosikia lakini bado wakaasi? Je, si wale wote waliotoka Misri wakiongozwa na Mose? [17] Lakini ni nani aliowakasirikia miaka arobaini? Je, si wale waliofanya dhambi ambao miili yao ilianguka jangwani? [18] Ni nani hao ambao Mungu aliapa kuwa kamwe hawataingia rahani mwake isipokuwa ni wale waliokataa kutii? [19] Hivyo tunaona kwamba hawakuweza kuingia kwa sababu ya kutokuamini kwao.