[1] Neno alilosema Mungu kuhusu Ninawi. Kitabu cha maono cha Nahumu, Mwelkoshi. [2] BWANA ni mwenye wivu na Mungu mlipiza kisasi; BWANA hulipiza kisasi na amejaa ghadhabu. BWANA hulipiza kisasi juu ya watesi wake, naye anadumisha ghadhabu yake dhidi ya adui zake. [3] BWANA si mwepesi wa hasira naye ni mwenye nguvu, BWANA hataacha kuadhibu wenye hatia. Njia yake ipo katika kisulisuli na tufani, na mawingu ni vumbi la miguu yake. [4] Anakemea bahari na kuikausha, anafanya mito yote kukauka. Bashani na Karmeli zinanyauka na maua ya Lebanoni hukauka. [5] Milima hutikisika mbele yake na vilima huyeyuka. Nchi hutetemeka mbele yake, dunia na wote waishio ndani yake. [6] Ni nani awezaye kuzuia hasira yake yenye uchungu? Nani awezaye kuvumilia hasira yake kali? Ghadhabu yake imemiminwa kama moto, na miamba inapasuka mbele zake. [7] BWANA ni Mwema, kimbilio wakati wa taabu. Huwatunza wale wanaomtegemea, [8] lakini kwa mafuriko makubwa, ataangamiza Ninawi; atafuatilia adui zake hadi gizani. [9] Shauri baya lolote wapangalo dhidi ya BWANA yeye atalikomesha; taabu haitatokea mara ya pili. [10] Watasongwa katikati ya miiba na kulewa kwa mvinyo wao. Watateketezwa kama mabua makavu. [11] Ee Ninawi, kutoka kwako amejitokeza mmoja, ambaye anapanga shauri baya dhidi ya BWANA na kushauri uovu. [12] Hili ndilo asemalo BWANA: “Ingawa wana muungano nao ni wengi sana, watakatiliwa mbali na kuangamia. Ingawa nimekutesa wewe, ee Yuda, sitakutesa tena. [13] Sasa nitavunja nira zao kutoka shingo yako, nami nitazivunjilia mbali pingu zako.” [14] Hii ndiyo amri BWANA aliyoitoa kukuhusu wewe, Ninawi: “Hutakuwa na wazao watakaoendeleza jina lako. Nitaharibu sanamu za kuchonga na sanamu za kuyeyusha ambazo zipo katika hekalu la miungu yenu. Nitaandaa kaburi lako, kwa maana wewe ni mwovu kabisa.” [15] Tazama, huko juu milimani, miguu ya huyo mmoja aletaye habari njema, ambaye anatangaza amani! Ee Yuda, sherehekea sikukuu zako, nawe utimize nadhiri zako. Waovu hawatakuvamia tena; wataangamizwa kabisa.