Mithali 31:1-31 ONEN
[1] Misemo ya Mfalme Lemueli, usia wa mama yake aliyomfundisha: [2] “Ee mwanangu, ee mwana wa tumbo langu, ee mwana wa nadhiri zangu, [3] Usitumie nguvu zako kwa wanawake, uhodari wako kwa wale wanaowaharibu wafalme. [4] “Ee Lemueli, haifai wafalme, haifai wafalme kunywa mvinyo, haifai watawala kutamani sana kileo, [5] wasije wakanywa na kusahau vile sheria inavyoamuru na kuwanyima haki zao wote walioonewa. [6] Wape kileo wale wanaoangamia, mvinyo wale walio na uchungu, [7] Wanywe na kusahau umaskini wao na wasikumbuke taabu yao tena. [8] “Sema kwa ajili ya wale wasioweza kujisemea, kwa ajili ya haki za wote walioachwa ukiwa. [9] Sema na uamue kwa haki, tetea haki za maskini na wahitaji.” [10] Mke mwenye sifa nzuri, ni nani awezaye kumpata? Yeye ni wa thamani sana kuliko marijani. [11] Mume wake anamwamini kikamilifu wala hakosi kitu chochote cha thamani. [12] Humtendea mumewe mema, wala si mabaya, siku zote za maisha yake. [13] Huchagua sufu na kitani naye hufanya kazi kwa mikono yenye bidii. [14] Yeye ni kama meli za biashara akileta chakula chake kutoka mbali. [15] Yeye huamka kungali bado giza huwapa jamaa yake chakula na mafungu kwa watumishi wake wa kike. [16] Huangalia shamba na kulinunua, kutokana na mapato yake hupanda shamba la mizabibu. [17] Hufanya kazi zake kwa nguvu, mikono yake ina nguvu kwa ajili ya kazi zake. [18] Huona kwamba biashara yake ina faida, wala taa yake haizimiki usiku. [19] Huweka mikono yake kwenye pia, navyo vidole vyake hushikilia kijiti chenye uzi. [20] Huwanyooshea maskini mikono yake na kuwakunjulia wahitaji vitanga vyake. [21] Theluji ishukapo, hana hofu kwa ajili ya watu wa nyumbani mwake, kwa maana wote wamevikwa nguo za kutia joto. [22] Hutengeneza mazulia ya urembo ya kufunika kitanda chake, yeye huvaa kitani safi na urujuani. [23] Mume wake anaheshimiwa kwenye lango la mji, aketipo miongoni mwa wazee wa nchi. [24] Hutengeneza mavazi ya kitani na kuyauza, naye huwauzia wafanyabiashara mishipi. [25] Amevikwa nguvu na heshima, anaweza kucheka bila kuwa na hofu kwa siku zijazo. [26] Huzungumza kwa hekima na mafundisho ya kuaminika yapo ulimini mwake. [27] Huangalia mambo ya nyumbani mwake wala hali chakula cha uvivu. [28] Watoto wake huamka na kumwita aliyebarikiwa, mumewe pia humsifu, akisema: [29] “Wanawake wengi hufanya vitu vyenye sifa nzuri, lakini wewe umewapita wote.” [30] Kujipamba ili kuvutia ni udanganyifu na uzuri unapita upesi, bali mwanamke anayemcha BWANA atasifiwa. [31] Mpe thawabu anayostahili, nazo kazi zake na zimletee sifa kwenye lango la mji.
