[1] Mkumbuke Muumba wako siku za ujana wako, kabla hazijaja siku za taabu, wala haijakaribia miaka utakaposema, “Mimi sifurahii hiyo”: [2] kabla jua na nuru, nao mwezi na nyota havijatiwa giza, kabla ya kurudi mawingu baada ya mvua; [3] siku ile walinzi wa nyumba watakapotetemeka, nao watu wenye nguvu watakapojiinamisha, wakati wasagao watakapokoma kwa sababu ya uchache, nao wachunguliao madirishani kutiwa giza; [4] wakati milango ya kuingia barabarani itakapofungwa na sauti ya kusaga kufifia; wakati watu wataamshwa kwa sauti ya ndege, lakini nyimbo zao zote zikififia; [5] wakati watu watakapoogopa kilichoinuka juu na hatari zitakazokuwepo barabarani; wakati mlozi utakapochanua maua na panzi kujikokota nawe usiwe na shauku ya kitu chochote. Ndipo mwanadamu aiendea nyumba yake ya milele nao waombolezaji wakizunguka barabarani. [6] Mkumbuke Muumba wako: kabla haijakatika kamba ya fedha, au bakuli la dhahabu halijavunjika; kabla mtungi kuvunjika kwenye chemchemi, au gurudumu kuvunjika kisimani, [7] nayo mavumbi kurudi ardhini yalikotoka, na roho kurudi kwa Mungu aliyeitoa. [8] Mhubiri asema, “Ubatili! Ubatili! Kila kitu ni ubatili!” [9] Mhubiri hakuwa tu na hekima, bali aliwagawia watu maarifa pia. Alitafakari na kutafiti na akaweka katika utaratibu mithali nyingi. [10] Mhubiri alitafiti ili kupata maneno sahihi na kila alichoandika kilikuwa sawa na kweli. [11] Maneno ya wenye hekima ni kama mchokoro, mithali zao zilizokusanywa pamoja ni kama misumari iliyogongomewa ikawa imara, yaliyotolewa na Mchungaji mmoja. [12] Tena zaidi ya hayo, mwanangu, kubali maonyo, hakuna mwisho wa kutunga vitabu vingi, nako kusoma sana huuchosha mwili. [13] Hii ndiyo jumla ya maneno; yote yamekwisha sikiwa: Mche Mungu, nawe uzishike amri zake, maana kwa jumla ndiyo impasayo mtu. [14] Kwa maana Mungu ataleta hukumuni kila kazi, pamoja na kila neno la siri, likiwa jema au baya.