Mathayo 4:1-25 ONEN
[1] Kisha Yesu akaongozwa na Roho Mtakatifu kwenda nyikani ili akajaribiwe na ibilisi. [2] Baada ya kufunga siku arobaini usiku na mchana, hatimaye akaona njaa. [3] Mjaribu akamjia na kumwambia, “Ikiwa wewe ndiye Mwana wa Mungu, amuru mawe haya yawe mikate.” [4] Lakini Yesu akajibu, “Imeandikwa: ‘Mtu haishi kwa mkate tu, ila kwa kila neno litokalo katika kinywa cha Mungu.’ ” [5] Ndipo ibilisi akamchukua Yesu mpaka mji mtakatifu na kumweka juu ya mnara mrefu wa Hekalu, [6] akamwambia, “Kama wewe ndiwe Mwana wa Mungu jitupe chini. Kwa kuwa imeandikwa: “ ‘Atakuagizia malaika zake, nao watakuchukua mikononi mwao ili usije ukajikwaa mguu wako katika jiwe.’ ” [7] Yesu akamjibu, “Pia imeandikwa: ‘Usimjaribu Bwana Mungu wako.’ ” [8] Kwa mara nyingine, ibilisi akamchukua Yesu mpaka kwenye kilele cha mlima mrefu na kumwonyesha falme zote za dunia na fahari zake, [9] kisha akamwambia, “Nitakupa hivi vyote kama ukinisujudia na kuniabudu.” [10] Yesu akamwambia, “Ondoka mbele yangu, Shetani! Kwa maana imeandikwa, ‘Mwabudu Bwana Mungu wako, na umtumikie yeye peke yake.’ ” [11] Ndipo ibilisi akamwacha, nao malaika wakaja na kumhudumia. [12] Yesu aliposikia kwamba Yohana Mbatizaji alikuwa ametiwa gerezani, alirudi Galilaya. [13] Akaondoka Nazareti akaenda kuishi Kapernaumu, mji ulioko karibu na bahari, katika mipaka ya nchi ya Zabuloni na Naftali, [14] ili kutimiza unabii wa nabii Isaya, kama alivyosema: [15] “Nchi ya Zabuloni na nchi ya Naftali, kwenye njia ya kuelekea baharini, ngʼambo ya Yordani, Galilaya ya watu wa Mataifa: [16] watu wale waliokaa gizani wameona nuru kuu; nao wale walioishi katika nchi ya uvuli wa mauti, nuru imewazukia.” [17] Tangu wakati huo, Yesu alianza kuhubiri akisema: “Tubuni, kwa maana Ufalme wa Mbinguni umekaribia.” [18] Yesu alipokuwa anatembea kando ya Bahari ya Galilaya, aliwaona ndugu wawili, Simoni aitwaye Petro, na Andrea ndugu yake. Walikuwa wakizitupa nyavu zao baharini kwa kuwa wao walikuwa wavuvi. [19] Yesu akawaambia, “Njooni, nifuateni nami nitawafanya mwe wavuvi wa watu.” [20] Mara wakaziacha nyavu zao, wakamfuata. [21] Alipoendelea mbele kutoka pale, akawaona ndugu wengine wawili, Yakobo mwana wa Zebedayo na Yohana nduguye, wakiwa wamekaa kwenye mashua pamoja na baba yao Zebedayo, wakizitengeneza nyavu zao. Yesu akawaita. [22] Nao mara wakaiacha mashua yao, pamoja na baba yao, wakamfuata. [23] Yesu akapita katika Galilaya yote, akifundisha katika masinagogi yao, akihubiri habari njema za Ufalme, na akiponya kila ugonjwa na kila aina ya maradhi miongoni mwa watu. [24] Kwa hiyo sifa zake zikaenea sehemu zote za Shamu, nao watu wakamletea wote waliokuwa na magonjwa mbalimbali na maumivu, waliopagawa na pepo wachafu, wenye kifafa na waliopooza, naye akawaponya. [25] Makutano makubwa ya watu yakawa yanamjia kutoka Galilaya, Dekapoli, Yerusalemu, Uyahudi na kutoka ngʼambo ya Mto Yordani.
