Mathayo 22:1-46 ONEN
[1] Yesu akasema nao tena kwa mifano, akawaambia, [2] “Ufalme wa Mbinguni unaweza kufananishwa na mfalme mmoja aliyemwandalia mwanawe karamu ya arusi. [3] Akawatuma watumishi wake kuwaita wale waliokuwa wamealikwa karamuni, lakini wakakataa kuja. [4] “Kisha akawatuma watumishi wengine akisema, ‘Waambieni wale walioalikwa kwamba nimeandaa chakula. Nimekwisha kuchinja mafahali wangu na vinono, karamu iko tayari. Karibuni kwa karamu ya arusi.’ [5] “Lakini hawakuzingatia, wakaenda zao: huyu shambani mwake na mwingine kwenye biashara zake. [6] Wengine wao wakawakamata wale watumishi wake, wakawatesa na kuwaua. [7] Yule mfalme akakasirika sana, akapeleka jeshi lake likawaangamiza wale wauaji na kuuteketeza mji wao kwa moto. [8] “Kisha akawaambia watumishi wake, ‘Karamu ya arusi imeshakuwa tayari, lakini wale niliowaalika hawakustahili kuja. [9] Kwa hiyo nendeni katika njia panda mkamwalike karamuni yeyote mtakayemwona.’ [10] Wale watumishi wakaenda barabarani, wakawakusanya watu wote waliowaona, wema na wabaya. Ukumbi wa arusi ukajaa wageni. [11] “Lakini mfalme alipoingia ndani ili kuwaona wageni, akamwona mle mtu mmoja ambaye hakuwa amevaa vazi la arusi. [12] Mfalme akamuuliza, ‘Rafiki, uliingiaje humu bila vazi la arusi?’ Yule mtu hakuwa na la kusema. [13] “Ndipo mfalme akawaambia watumishi wake, ‘Mfungeni mikono na miguu mkamtupe nje, kwenye giza. Huko kutakuwa na kilio na kusaga meno.’ [14] “Kwa maana walioitwa ni wengi, lakini walioteuliwa ni wachache.” [15] Ndipo Mafarisayo wakatoka nje wakaandaa mpango wa kumtega Yesu katika maneno yake. [16] Wakatuma wanafunzi wao kwake pamoja na Maherode. Nao wakasema, “Mwalimu, tunajua kwamba wewe ni mtu mwadilifu na unafundisha njia ya Mungu katika kweli bila kuyumbishwa na mtu wala kuonyesha upendeleo. [17] Tuambie basi, wewe unaonaje? Je, ni halali kulipa kodi kwa Kaisari, au la?” [18] Lakini Yesu, akijua makusudi yao mabaya, akawaambia, “Enyi wanafiki, kwa nini mnajaribu kunitega? [19] Nionyesheni hiyo sarafu inayotumika kwa kulipia kodi.” Wakamletea dinari. [20] Naye akawauliza, “Sura hii ni ya nani? Na maandishi haya ni ya nani?” [21] Wakamjibu, “Ni vya Kaisari.” Basi Yesu akawaambia, “Mpeni Kaisari kilicho cha Kaisari, naye Mungu mpeni kilicho cha Mungu.” [22] Waliposikia hili, wakashangaa. Hivyo wakamwacha, wakaenda zao. [23] Siku hiyo hiyo Masadukayo, wale wasemao kwamba hakuna ufufuo wa wafu, wakamjia Yesu na kumuuliza swali, wakisema, [24] “Mwalimu, Mose alisema, ‘Kama mtu akifa bila kuwa na watoto, ndugu yake inampasa amwoe huyo mjane ili ampatie watoto huyo nduguye aliyekufa.’ [25] Basi palikuwa na ndugu saba miongoni mwetu. Yule wa kwanza akaoa mke, naye akafa, na kwa kuwa hakuwa na watoto, akamwachia nduguye yule mjane. [26] Ikatokea vivyo hivyo kwa yule ndugu wa pili, na wa tatu, hadi wote saba. [27] Hatimaye, yule mwanamke naye akafa. [28] Sasa basi, siku ya ufufuo, yeye atakuwa mke wa nani miongoni mwa wale ndugu saba, kwa kuwa wote walikuwa wamemwoa huyo mwanamke?” [29] Yesu akawajibu, “Mwapotoka kwa sababu hamjui Maandiko wala uweza wa Mungu. [30] Wakati wa ufufuo, watu hawataoa wala kuolewa, bali watakuwa kama malaika wa mbinguni. [31] Lakini kuhusu ufufuo wa wafu, hamjasoma kile Mungu alichowaambia, kwamba, [32] ‘Mimi ni Mungu wa Abrahamu, Mungu wa Isaki, na Mungu wa Yakobo’? Yeye si Mungu wa wafu, bali ni Mungu wa walio hai.” [33] Ule umati wa watu uliposikia hayo, ulishangaa sana kwa mafundisho yake. [34] Mafarisayo waliposikia kwamba Yesu alikuwa amewanyamazisha Masadukayo, Mafarisayo wakakusanyika pamoja. [35] Mmoja wao, mtaalamu wa sheria, akamuuliza swali ili kumjaribu, akisema, [36] “Mwalimu, ni amri ipi katika Sheria iliyo kuu kuliko zote?” [37] Yesu akamjibu, “ ‘Mpende Bwana Mungu wako kwa moyo wako wote na kwa roho yako yote na kwa akili zako zote.’ [38] Hii ndiyo amri iliyo kuu, tena ni ya kwanza. [39] Nayo ya pili ni kama hiyo, nayo ni hii: ‘Mpende jirani yako kama nafsi yako.’ [40] Amri hizi mbili ndizo msingi wa Sheria na Manabii.” [41] Wakati Mafarisayo walikuwa wamekusanyika pamoja, Yesu akawauliza, [42] “Mnaonaje kuhusu Kristo? Yeye ni mwana wa nani?” Wakamjibu, “Yeye ni mwana wa Daudi.” [43] Akawaambia, “Inakuwaje basi kwamba Daudi, akinena kwa kuongozwa na Roho, anamwita Kristo ‘Bwana’? Kwa maana asema, [44] “ ‘BWANA alimwambia Bwana wangu: “Keti mkono wangu wa kuume, hadi nitakapowaweka adui zako chini ya miguu yako.” ’ [45] Kama basi Daudi anamwita yeye ‘Bwana,’ awezaje kuwa mwanawe?” [46] Hakuna mtu aliyeweza kumjibu Yesu neno. Tena tangu siku hiyo hakuna aliyethubutu kumuuliza tena maswali.
