[1] Kumbuka, Ee BWANA, yaliyotupata, tazama, nawe uione aibu yetu. [2] Urithi wetu umegeuziwa kwa wageni, na nyumba zetu kwa wageni. [3] Tumekuwa yatima wasio na baba, mama zetu wamekuwa kama wajane. [4] Ni lazima tununue maji tunayokunywa, kuni zetu zapatikana tu kwa kununua. [5] Wanaotufuatilia wapo kwenye visigino vyetu, tumechoka na hakuna pumziko. [6] Tumejitolea kwa Misri na Ashuru tupate chakula cha kutosha. [7] Baba zetu walitenda dhambi na hawapo tena, na sisi tunachukua adhabu yao. [8] Watumwa wanatutawala na hakuna wa kutuokoa mikononi yao. [9] Tunapata chakula chetu kwa kuhatarisha maisha yetu kwa sababu ya upanga jangwani. [10] Ngozi yetu ina joto kama tanuru, kwa sababu ya fadhaa itokanayo na njaa. [11] Wanawake wametendwa jeuri katika Sayuni, na mabikira katika miji ya Yuda. [12] Wakuu wametungikwa juu kwa mikono yao, wazee hawapewi heshima. [13] Vijana wanataabika kwenye mawe ya kusagia, wavulana wanayumbayumba chini ya mizigo ya kuni. [14] Wazee wameondoka langoni la mji, vijana wameacha kuimba nyimbo zao. [15] Furaha imeondoka mioyoni mwetu, kucheza kwetu kumegeuka maombolezo. [16] Taji imeanguka kutoka kichwani petu. Ole wetu, kwa maana tumetenda dhambi! [17] Kwa sababu hiyo, mioyo yetu inazimia, kwa sababu ya hayo, macho yetu yamefifia, [18] kwa ajili ya Mlima Sayuni, ambao unakaa ukiwa, nao mbweha wanatembea juu yake. [19] Wewe, Ee BWANA unatawala milele, kiti chako cha enzi chadumu kizazi hadi kizazi. [20] Kwa nini watusahau siku zote? Kwa nini umetuacha kwa muda mrefu? [21] Turudishe kwako mwenyewe, Ee BWANA, ili tupate kurudi. Zifanye mpya siku zetu kama siku za kale, [22] isipokuwa uwe umetukataa kabisa na umetukasirikia pasipo kipimo.