Maombolezo 3:1-66 ONEN
[1] Mimi ndiye mtu aliyeona mateso kwa fimbo ya ghadhabu yake. [2] Amenifukuzia mbali na kunifanya nitembee gizani wala si katika nuru; [3] hakika, amegeuza mkono wake dhidi yangu tena na tena, mchana kutwa. [4] Amefanya ngozi yangu na nyama yangu kuchakaa na ameivunja mifupa yangu. [5] Amenizingira na kunizunguka kwa uchungu na taabu. [6] Amenifanya niishi gizani kama wale waliokufa. [7] Amenizungushia ukuta ili nisiweze kutoroka, amenifunga kwa minyororo mizito. [8] Hata ninapoita au kulia ili kuomba msaada, anakataa kupokea maombi yangu. [9] Ameizuia njia yangu kwa mapande ya mawe, amepotosha njia zangu. [10] Kama dubu aviziaye, kama simba mafichoni, [11] ameniburuta kutoka njia, akanirarua na kuniacha bila msaada. [12] Amevuta upinde wake na kunifanya mimi niwe lengo kwa ajili ya mishale yake. [13] Alinichoma moyo wangu kwa mishale iliyotoka kwenye podo lake. [14] Nimekuwa kichekesho kwa watu wangu wote, wananidhihaki kwa wimbo mchana kutwa. [15] Amenijaza kwa majani machungu na kunishibisha kwa nyongo. [16] Amevunja meno yangu kwa changarawe, amenikanyagia mavumbini. [17] Amani yangu imeondolewa, nimesahau kufanikiwa ni nini. [18] Kwa hiyo nasema, “Fahari yangu imeondoka na yale yote niliyokuwa nimetarajia kutoka kwa BWANA.” [19] Nayakumbuka mateso yangu na kutangatanga kwangu, uchungu na nyongo. [20] Ninayakumbuka vyema, nayo nafsi yangu imezimia ndani yangu. [21] Hata hivyo najikumbusha neno hili na kwa hiyo ninalo tumaini. [22] Kwa sababu ya upendo mkuu wa BWANA, hatuangamii, kwa kuwa huruma zake hazikomi kamwe. [23] Ni mpya kila asubuhi, uaminifu wako ni mkuu. [24] Nimeiambia nafsi yangu, “BWANA ni fungu langu, kwa hiyo nitamngojea.” [25] BWANA ni mwema kwa wale ambao tumaini lao ni kwake, kwa yule ambaye humtafuta; [26] ni vyema kungojea kwa utulivu kwa ajili ya wokovu wa BWANA. [27] Ni vyema mtu kuchukua nira bado angali kijana. [28] Na akae peke yake awe kimya, kwa maana BWANA ameiweka juu yake. [29] Na azike uso wake mavumbini bado panawezekana kuwa na matumaini. [30] Na atoe shavu lake kwa yule ampigaye, na ajazwe na aibu. [31] Kwa kuwa watu hawakatiliwi mbali na Bwana milele. [32] Ingawa huleta huzuni, ataonyesha huruma, kwa kuwa upendo wake usiokoma ni mkuu. [33] Kwa maana hapendi kuwaletea mateso au huzuni watoto wa wanadamu. [34] Kuwaponda chini ya nyayo wafungwa wote katika nchi, [35] Kumnyima mtu haki zake mbele za Aliye Juu Sana, [36] kumnyima mtu haki: Je, Bwana asione mambo kama haya? [37] Nani awezaye kusema nalo likatendeka kama Bwana hajaamuru? [38] Je, si ni kwenye kinywa cha Aliye Juu Sana ndiko yatokako maafa na mambo mema? [39] Mwanadamu yeyote aliye hai aweza kulalamika wakati anapoadhibiwa kwa ajili ya dhambi zake? [40] Tuzichunguze njia zetu na kuzijaribu, na tumrudie BWANA Mungu. [41] Tuinue mioyo yetu pamoja na mikono yetu kwa Mungu mbinguni, na tuseme: [42] “Tumetenda dhambi na kuasi nawe hujasamehe. [43] “Umejifunika mwenyewe kwa hasira na kutufuatilia; umetuchinja bila huruma. [44] Unajifunika mwenyewe kwa wingu, ili pasiwe na ombi litakaloweza kupenya. [45] Umetufanya takataka na uchafu miongoni mwa mataifa. [46] “Adui zetu wote wamefumbua vinywa vyao wazi dhidi yetu. [47] Tumeteseka kwa hofu kuu na shida ya ghafula, uharibifu na maangamizi.” [48] Vijito vya machozi vinatiririka kutoka machoni mwangu, kwa sababu watu wangu wameangamizwa. [49] Macho yangu yatatiririka machozi bila kukoma, bila kupata nafuu, [50] hadi BWANA atazame chini kutoka mbinguni na kuona. [51] Lile ninaloliona huniletea huzuni nafsini kwa sababu ya wanawake wote wa mji wangu. [52] Wale waliokuwa adui zangu bila sababu wameniwinda kama ndege. [53] Walijaribu kukomesha maisha yangu ndani ya shimo na kunitupia mawe; [54] maji yalifunika juu ya kichwa changu, nami nikafikiri nilikuwa karibu kukatiliwa mbali. [55] Nililiitia jina lako, Ee BWANA, kutoka vina vya shimo. [56] Ulisikia ombi langu: “Usikizibie masikio yako kilio changu nikuombapo msaada.” [57] Ulikuja karibu nilipokuita, nawe ukasema, “Usiogope.” [58] Ee Bwana, ulichukua shauri langu, ukaukomboa uhai wangu. [59] Umeona, Ee BWANA, ubaya niliotendewa. Tetea shauri langu! [60] Umeona kina cha kisasi chao, mashauri yao yote mabaya dhidi yangu. [61] Ee BWANA, umesikia matukano yao, mashauri yao yote mabaya dhidi yangu: [62] kile adui zangu wanachonongʼona na kunungʼunikia dhidi yangu mchana kutwa. [63] Watazame! Wakiwa wameketi au wamesimama, wananidhihaki katika nyimbo zao. [64] Uwalipe kile wanachostahili, Ee BWANA, kwa yale ambayo mikono yao imetenda. [65] Weka pazia juu ya mioyo yao, laana yako na iwe juu yao! [66] Wafuatilie katika hasira na uwaangamize kutoka chini ya mbingu za BWANA.
