Kutoka 6:1-30 ONEN
[1] Kisha BWANA akamwambia Mose, “Sasa utaona kitu nitakachomfanyia Farao: Kwa sababu ya mkono wangu wenye nguvu atawaachia watu waende; kwa sababu ya mkono wangu wenye nguvu atawafukuza waondoke nchini mwake.” [2] Pia Mungu akamwambia Mose, “Mimi ndimi BWANA. [3] Nilimtokea Abrahamu, Isaki na Yakobo kama Mungu Mwenyezi, ingawa sikuwajulisha Jina langu, Yehova, Mimi mwenyewe sikujitambulisha kwao. [4] Pia niliweka Agano langu nao kuwapa nchi ya Kanaani, ambako waliishi kama wageni. [5] Zaidi ya hayo, nimesikia kilio cha huzuni cha Waisraeli ambao Wamisri wamewatia utumwani, nami nimelikumbuka Agano langu. [6] “Kwa hiyo, waambie Waisraeli: ‘Mimi ndimi BWANA, nami nitawatoa mtoke katika kongwa la Wamisri. Nitawaweka huru mtoke kuwa watumwa wao, nami nitawakomboa kwa mkono ulionyooshwa pamoja na matendo makuu ya hukumu. [7] Nitawatwaa mwe watu wangu mwenyewe, nami nitakuwa Mungu wenu. Ndipo mtajua kuwa mimi ndimi BWANA Mungu wenu, niliyewatoa chini ya kongwa la Wamisri. [8] Nami nitawaleta mpaka nchi niliyoapa kwa mkono ulioinuliwa kumpa Abrahamu, Isaki na Yakobo. Nitawapa iwe milki yenu. Mimi ndimi BWANA.’ ” [9] Mose akawaarifu Waisraeli jambo hili, lakini hawakumsikiliza kwa sababu ya maumivu makuu ya moyoni na utumwa wa kikatili. [10] Ndipo BWANA akamwambia Mose, [11] “Nenda, mwambie Farao mfalme wa Misri awaachie Waisraeli waondoke nchini mwake.” [12] Lakini Mose akamwambia BWANA, “Ikiwa Waisraeli hawatanisikiliza, kwa nini yeye Farao anisikilize mimi, ambaye huzungumza kwa kigugumizi?” [13] Ndipo BWANA akanena na Mose na Aroni kuhusu Waisraeli na Farao mfalme wa Misri, naye akawaamuru wawatoe Waisraeli kutoka Misri. [14] Hawa walikuwa wakuu wa jamaa zao: Wana wa Reubeni mzaliwa wa kwanza wa kiume wa Israeli walikuwa Hanoki, Palu, Hesroni na Karmi. Hawa walikuwa ndio koo za Reubeni. [15] Wana wa Simeoni walikuwa Yemueli, Yamini, Ohadi, Yakini, Sohari na Shauli mwana wa mwanamke Mkanaani. Hawa walikuwa ndio koo za Simeoni. [16] Haya ndiyo majina ya wana wa Lawi kufuatana na orodha zao: Gershoni, Kohathi na Merari. Lawi aliishi miaka 137. [17] Wana wa Gershoni kwa koo, walikuwa Libni na Shimei. [18] Wana wa Kohathi walikuwa Amramu, Ishari, Hebroni na Uzieli. Kohathi aliishi miaka 133. [19] Wana wa Merari walikuwa Mahli na Mushi. Hizi ndizo zilizokuwa koo za Lawi kufuatana na orodha zao. [20] Amramu akamwoa Yokebedi, shangazi yake, ambaye alimzalia Aroni na Mose. Amramu aliishi miaka 137. [21] Wana wa Ishari walikuwa Kora, Nefegi na Zikri. [22] Wana wa Uzieli walikuwa Mishaeli, Elisafani na Sithri. [23] Aroni akamwoa Elisheba binti wa Aminadabu ndugu yake Nashoni, naye akamzalia Nadabu, Abihu, Eleazari na Ithamari. [24] Wana wa Kora walikuwa Asiri, Elikana na Abiasafu. Hawa walikuwa ndio koo za Kora. [25] Eleazari mwana wa Aroni akamwoa mmoja wa binti za Putieli, naye akamzalia Finehasi. Hawa walikuwa ndio wakuu wa jamaa za Walawi, ukoo kwa ukoo. [26] Hawa walikuwa Aroni na Mose wale wale ambao BWANA aliwaambia, “Watoeni Waisraeli katika nchi ya Misri kwa vikosi vyao.” [27] Ndio hao hao waliozungumza na Farao mfalme wa Misri kuhusu kuwatoa Waisraeli Misri. Ilikuwa ni huyo Mose na huyo Aroni. [28] BWANA aliponena na Mose huko Misri, [29] akamwambia, “Mimi ndimi BWANA. Mwambie Farao mfalme wa Misri kila kitu nikuambiacho.” [30] Lakini Mose akamwambia BWANA, “Kwa kuwa mimi huzungumza kwa kigugumizi, Farao atanisikiliza mimi?”
