Kumbukumbu 6:1-25 ONEN
[1] Haya ndiyo maagizo, amri na sheria ambazo BWANA Mungu wenu aliniagiza niwafundishe ninyi ili mpate kuyashika katika nchi ambayo ninyi mnavuka Yordani kuimiliki, [2] ili kwamba ninyi, watoto wenu na watoto wao baada yao wamche BWANA Mungu wenu siku zote kwa kushika amri na maagizo yake yote ninayowapa, ili mweze kuyafurahia maisha marefu. [3] Sikia, ee Israeli, nawe uwe mwangalifu kutii ili upate kufanikiwa na kuongezeka sana katika nchi itiririkayo maziwa na asali, kama BWANA, Mungu wa baba zenu, alivyowaahidi ninyi. [4] Sikia, ee Israeli: BWANA Mungu wako, BWANA ni mmoja. [5] Mpende BWANA Mungu wako kwa moyo wako wote, na kwa roho yako yote, na kwa nguvu zako zote. [6] Amri hizi ninazokupa leo zitakuwa katika moyo wako. [7] Wafundishe watoto wako kwa bidii. Nena kuhusu amri hizi uketipo nyumbani na wakati utembeapo njiani, ulalapo na uamkapo. [8] Zifunge kama alama juu ya mkono wako, na uzifunge juu ya paji la uso wako. [9] Ziandike kwenye miimo ya milango ya nyumba yako na juu ya malango yako. [10] Wakati BWANA Mungu wako atakapokuleta katika nchi aliyowaapia baba zako, Abrahamu, Isaki na Yakobo, kukupa wewe, nchi kubwa, ina miji inayopendeza ambayo hukuijenga, [11] nyumba zilizojaa vitu vizuri vya aina nyingi ambavyo hukuvijaza, visima ambavyo hukuchimba, na mashamba ya mizabibu na mizeituni ambayo hukupanda wewe, basi, utakapokula na kushiba, [12] jihadhari usije ukamwacha BWANA, aliyekutoa katika nchi ya Misri, kutoka nchi ya utumwa. [13] Utamcha BWANA Mungu wako, na umtumikie yeye peke yake na kuapa kwa jina lake. [14] Usifuate miungu mingine, miungu ya mataifa yanayokuzunguka; [15] kwa kuwa BWANA Mungu wako, ambaye yuko katikati yako, ni Mungu mwenye wivu na hasira yake itawaka dhidi yako, naye atakuangamiza kutoka uso wa nchi. [16] Usimjaribu BWANA Mungu wako kama ulivyofanya huko Masa. [17] Utayashika maagizo ya BWANA Mungu wako kwa bidii, na masharti na amri alizokupa. [18] Fanya lililo haki na jema mbele za BWANA, ili upate kufanikiwa, uweze kuingia na kuimiliki nchi nzuri ambayo BWANA aliahidi kwa kiapo kwa baba zako, [19] kuwafukuza kwa nguvu adui zako mbele yako kama BWANA alivyosema. [20] Siku zijazo, mtoto wako atakapokuuliza, “Ni nini maana ya masharti haya, amri na sheria hizi ambazo BWANA Mungu wako alikuagiza wewe?” [21] Mwambie: “Tulikuwa watumwa wa Farao huko Misri, lakini BWANA alitutoa sisi kutoka Misri kwa mkono wenye nguvu. [22] BWANA akapeleka mbele yetu ishara za miujiza na maajabu makubwa na ya kutisha mno juu ya Misri na Farao pamoja na nyumba yake yote. [23] Lakini Mungu akatutoa huko, akatuleta na kutupa nchi hii ambayo aliwaahidi baba zetu kwa kiapo. [24] BWANA akatuagiza tutii amri hizi zote na kumcha BWANA Mungu wetu, ili tupate kustawi na kuendelea kuwa hai kama ilivyo leo. [25] Kama tukizitii kwa bidii amri hizi zote mbele za BWANA Mungu wetu, kama alivyotuamuru sisi, hiyo itakuwa haki yetu.”
