[1] Kisha Mose akaupanda mlima Nebo kutoka tambarare za Moabu mpaka kilele cha Pisga, ngʼambo ya Yeriko. Huko BWANA akamwonyesha nchi yote: kutoka Gileadi mpaka Dani, [2] Naftali yote, nchi ya Efraimu na Manase, nchi yote ya Yuda mpaka bahari ya magharibi, [3] Negebu na nchi yote kuanzia Bonde la Yeriko, Mji wa Mitende, hadi Soari. [4] Kisha BWANA akamwambia, “Hii ndiyo nchi niliyomwahidi Abrahamu na Isaki na Yakobo kwa kiapo niliposema, ‘Nitawapa wazao wako.’ Nimekuruhusu uione kwa macho yako, lakini hutavuka kuingia.” [5] Naye Mose mtumishi wa BWANA akafa huko Moabu, kama BWANA alivyokuwa amesema. [6] Mungu akamzika huko Moabu, katika bonde mkabala na Beth-Peori, lakini hakuna ajuaye kaburi lake lilipo mpaka leo. [7] Mose alikuwa na umri wa miaka mia moja na ishirini alipofariki; hata hivyo nguvu ya macho yake haikufifia wala mwili wake haukudhoofika. [8] Waisraeli wakaomboleza kwa ajili ya Mose kwenye tambarare za Moabu kwa siku thelathini, mpaka wakati wa kulia na kuomboleza ulipopita. [9] Basi Yoshua mwana wa Nuni alijazwa roho ya hekima kwa sababu Mose alikuwa ameweka mikono yake juu yake. Kwa hiyo Waisraeli wakamsikiliza na wakafanya yale ambayo BWANA alikuwa amemwagiza Mose. [10] Tangu wakati huo, katika Israeli hajainuka nabii mwingine kama Mose, ambaye BWANA alimjua uso kwa uso, [11] aliyetenda ishara zote zile za miujiza na maajabu ambayo BWANA alimtuma kuyatenda huko Misri, yaani kwa Farao na maafisa wake wote na nchi yake yote. [12] Kwa kuwa hakuna mtu yeyote aliyewahi kuonyesha nguvu nyingi ama kutenda matendo ya kutisha ambayo Mose aliwahi kuyafanya mbele ya Israeli yote.