Kumbukumbu 10:1-22 ONEN
[1] Wakati ule BWANA aliniambia, “Chonga vibao viwili vya mawe kama vile vya kwanza uje kwangu juu mlimani. Pia utengeneze Sanduku la mbao. [2] Nitaandika juu ya vibao maneno yaliyokuwa katika vile vibao vya kwanza, ambavyo ulivivunja. Kisha utaviweka ndani ya Sanduku.” [3] Hivyo nikatengeneza Sanduku kwa mti wa mshita, nikachonga pia vibao vya mawe kama vile vya kwanza, kisha nikakwea mlimani nikiwa na vibao viwili mikononi mwangu. [4] BWANA akaandika juu ya hivi vibao kile alichokuwa amekiandika kabla, Amri Kumi alizokuwa amewatangazia juu mlimani, kutoka kwenye moto siku ile ya kusanyiko. BWANA akanikabidhi. [5] Kisha nikashuka kutoka mlimani na kuweka vibao ndani ya Sanduku nililokuwa nimelitengeneza, kama BWANA alivyoniagiza, navyo viko huko sasa. [6] (Waisraeli walisafiri kutoka visima vya Yaakani hadi Mosera. Huko Aroni alifariki na kuzikwa, naye Eleazari mwanawe akachukua nafasi yake kama kuhani. [7] Kutoka pale, walisafiri hadi Gudgoda wakaendelea mpaka Yotbatha, nchi yenye vijito vya maji. [8] Wakati huo BWANA aliteua kabila la Lawi kulibeba Sanduku la Agano la BWANA, kusimama mbele za BWANA ili kutoa huduma, na kutangaza baraka kwa Jina lake, kama wanavyofanya mpaka leo. [9] Hiyo ndiyo sababu ya Walawi kutokuwa na sehemu wala urithi miongoni mwa ndugu zao; BWANA ndiye urithi wao, kama BWANA Mungu wao alivyowaambia.) [10] Basi nilikaa mlimani kwa siku arobaini usiku na mchana, kama nilivyofanya mara ya kwanza, pia BWANA alinisikiliza hata wakati huu. Haikuwa nia yake kuwaangamiza. [11] BWANA akaniambia, “Nenda, ukawaongoze watu katika njia yao ili kwamba waweze kuingia na kuimiliki nchi ile niliyowaapia baba zao kuwapa.” [12] Na sasa, ee Israeli, BWANA Mungu wako anataka nini kwako ila kumcha BWANA Mungu wako, kwenda katika njia zake, kumpenda na kumtumikia BWANA Mungu wako kwa moyo wako wote na kwa roho yako yote, [13] na kuyashika maagizo ya BWANA na amri zake ninazokupa leo kwa mafanikio yako mwenyewe? [14] Mbingu, hata mbingu za juu sana, dunia na kila kitu kilichomo ndani yake, ni mali ya BWANA Mungu wako. [15] Hata hivyo BWANA alikuwa na shauku na baba zako, akawapenda na akawachagua ninyi, wazao wao, kuliko mataifa yote, kama ilivyo leo. [16] Kwa hiyo tahirini mioyo yenu, na msiwe na shingo ngumu tena. [17] Kwa kuwa BWANA Mungu wenu ni Mungu wa miungu na Bwana wa mabwana, Mungu mkuu, mwenye uweza na wa kutisha, ambaye hana upendeleo na hapokei rushwa. [18] Huwapigania yatima na wajane, humpenda mgeni, akimpa chakula na mavazi. [19] Nanyi wapendeni wageni, kwa kuwa ninyi wenyewe mlikuwa wageni huko Misri. [20] Mche BWANA Mungu wako na umtumikie yeye. Shikamana naye kwa uthabiti na kuapa kwa jina lake. [21] Yeye ni sifa yako; yeye ni Mungu wako, ambaye alikutendea yale maajabu makubwa na ya kutisha uliyoyaona kwa macho yako mwenyewe. [22] Baba zako walioshuka kwenda Misri jumla yao walikuwa sabini, na sasa BWANA Mungu wako amekufanya wengi kama nyota za angani.
