[1] Kwa ajili ya Sayuni sitanyamaza, kwa ajili ya Yerusalemu sitatulia, mpaka haki yake itakapoangaza kama mapambazuko, wokovu wake kama mwanga wa moto. [2] Mataifa wataona haki yako, nao wafalme wote wataona utukufu wako; wewe utaitwa kwa jina jipya lile ambalo kinywa cha BWANA kitatamka. [3] Utakuwa taji ya fahari mkononi mwa BWANA, taji ya kifalme mkononi mwa Mungu wako. [4] Hawatakuita tena Aliyeachwa, wala nchi yako kuiita Ukiwa. Bali utaitwa Hefsiba, nayo nchi yako itaitwa Beula, kwa maana BWANA atakufurahia, nayo nchi yako itaolewa. [5] Kama vile kijana aoavyo mwanamwali, ndivyo wanao watakavyokuoa wewe; kama bwana arusi amfurahiavyo bibi arusi wake, ndivyo Mungu wako atakavyokufurahia wewe. [6] Nimeweka walinzi juu ya kuta zako, ee Yerusalemu, hawatanyamaza mchana wala usiku. Ninyi wenye kumwita BWANA, msitulie, [7] msimwache apumzike hadi atakapoufanya imara Yerusalemu na kuufanya uwe sifa ya dunia. [8] BWANA ameapa kwa mkono wake wa kuume na kwa mkono wake wenye nguvu: “Kamwe sitawapa tena adui zenu nafaka zenu kama chakula chao; kamwe wageni hawatakunywa tena divai mpya ambayo mmeitaabikia, [9] lakini wale waivunao nafaka wataila na kumsifu BWANA, nao wale wakusanyao zabibu watainywa divai yake katika nyua za patakatifu pangu.” [10] Piteni, piteni katika malango! Tengenezeni njia kwa ajili ya watu. Jengeni, jengeni njia kuu! Ondoeni mawe. Inueni bendera kwa ajili ya mataifa. [11] BWANA ametoa tangazo mpaka miisho ya dunia: “Mwambie Binti Sayuni, ‘Tazama, mwokozi wako anakuja! Tazama ujira wake uko pamoja naye, na malipo yake yanafuatana naye!’ ” [12] Wataitwa Watu Watakatifu, Waliokombolewa na BWANA; nawe utaitwa Aliyetafutwa, Mji Usioachwa Tena.