[1] Amka, amka, ee Sayuni, jivike nguvu. Vaa mavazi yako ya fahari, ee Yerusalemu, mji mtakatifu. Asiyetahiriwa na aliye najisi hataingia kwako tena. [2] Jikungʼute mavumbi yako, inuka, uketi kwenye kiti cha enzi, ee Yerusalemu. Jifungue minyororo iliyo shingoni mwako, ee Binti Sayuni uliye mateka. [3] Kwa kuwa hili ndilo asemalo BWANA: “Mliuzwa pasipo malipo, nanyi mtakombolewa bila fedha.” [4] Kwa maana hili ndilo asemalo BWANA Mwenyezi: “Hapo kwanza watu wangu walishuka Misri kuishi, hatimaye, Ashuru wakawaonea. [5] “Basi sasa nina nini hapa?” asema BWANA. “Kwa kuwa watu wangu wamechukuliwa pasipo malipo, nao wale wanaowatawala wanawadhihaki,” asema BWANA. “Mchana kutwa jina langu limetukanwa bila kikomo. [6] Kwa hiyo watu wangu watalijua Jina langu; kwa hiyo katika siku ile watajua kwamba ndimi niliyetangulia kulisema. Naam, ni mimi.” [7] Tazama jinsi miguu ya wale waletao habari njema ilivyo mizuri juu ya milima, wale wanaotangaza amani, wanaoleta habari njema, wanaotangaza wokovu, wauambiao Sayuni, “Mungu wako anatawala!” [8] Sikiliza! Walinzi wako wanapaza sauti zao, pamoja wanapaza sauti zao kwa furaha. Wakati BWANA atakaporejea Sayuni, wataliona kwa macho yao wenyewe. [9] Pazeni sauti ya nyimbo za furaha pamoja, enyi magofu ya Yerusalemu, kwa maana BWANA amewafariji watu wake, ameikomboa Yerusalemu. [10] Mkono mtakatifu wa BWANA umefunuliwa machoni pa mataifa yote, nayo miisho yote ya dunia itaona wokovu wa Mungu wetu. [11] Ondokeni, ondokeni, tokeni huko! Msiguse kitu chochote kilicho najisi! Tokeni kati yake mwe safi, ninyi mchukuao vyombo vya BWANA. [12] Lakini hamtaondoka kwa haraka, wala hamtakwenda kwa kukimbia; kwa maana BWANA atatangulia mbele yenu, Mungu wa Israeli atakuwa mlinzi nyuma yenu. [13] Tazama, mtumishi wangu atatenda kwa hekima; atatukuzwa, na kuinuliwa juu, na kukwezwa sana. [14] Kama walivyokuwa wengi walioshangazwa naye, kwani uso wake ulikuwa umeharibiwa sana zaidi ya mtu yeyote na umbo lake kuharibiwa zaidi ya mfano wa mwanadamu: [15] hivyo atayashangaza mataifa mengi, nao wafalme watafunga vinywa vyao kwa sababu yake. Kwa kuwa yale ambayo hawakuambiwa, watayaona, nayo yale wasiyoyasikia, watayafahamu.